• VIPINDI VYA ELIMU HASA KILIMO

    Tuna vipindi mbalimbali vinavyohamasisha jamii katika kilimo cha Korosho, ufuta na Mhogo. tunaendelea na jamii inafurahia uwepo wa vipindi kwa sababu wanakutana na wataalamu moja kwa moja

  • SAUTI ZA WANAJAMII HUSIKIKA

    Sauti ni muhimu hasa unapohudumia jamii ya vijijini, wasikilizaji hupenda kusikia sauti zao kwakua watu wao wanawafahamu, hivyo huwa kivutio kwako na ni rahisi jamii kuamini kuwa mpo pamoja nao

  • MICHEZO MBALIMBALI

    Afya ni sehemu ya vipindi vyetu kwenye radio, hii husaidia kuwapa fursa watu wanaopenda michezo kuwa pamoja na kubadirishana mawazo, michezo hujenga urafiki na undugu baina mwa jamii

  • WATOTO KATIKA RADIO

    Hupenda kushiriki na hujiona sehemu ya radio kwa kuwa huishi katika jamii, kipindi cha watoto kimekuwa kikifuatiliwa na watu wazima kwasababu kuu moja tu, watoto waishio vijijini huwa hawapewi kipaumbele kama tulivyofanya Jamii fm

  • SIKIKA KATIKA RADIO

    Kipengere hiki hutoa fursa kwa wanajamii wanaotuzunguka kuongea moja kwa moja na kueleza hoja zao ambazo baadae hufuatiliwa kwa undani

13 mbaloni kwa wizi wa pembejeo za korosho

 

Kamanda wa Polisi mkoa wa Mtwara SACP Issa Suleiman akizungumza na Waandishi habari juu ya tukio la kukamatwa kwa watu 13 wanaotuhumiwa kwa wizi wa Pembejeo (Picha na Musa Mtepa)

Jeshi la Polisi Mtwara linawashikilia watuhumiwa 13 kwa tuhuma za wizi wa pembejeo za korosho zilizotolewa kwa wakulima msimu wa 2024/2025, wakiwemo watendaji wa serikali

Na Musa Mtepa

Mtwara, Septemba 10, 2025 – Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara linawashikilia watu 13 kwa tuhuma za kuhusika na wizi wa pembejeo za kilimo zilizotolewa kwa wakulima wa korosho katika msimu wa mwaka 2024/2025.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mtwara, SACP Issa Suleiman, amesema watuhumiwa hao walikamatwa Agosti 29, 2025 kufuatia operesheni maalum iliyoendeshwa kwa ushirikiano kati ya vyombo vya ulinzi na usalama na Bodi ya Korosho Tanzania (CBT).

Sauti ya 1 SACP Issa Suleima RPC Mtwara

Kamanda huyo pia ametoa rai kwa viongozi wa vyama vya ushirika pamoja na wananchi kwa ujumla kuacha vitendo vya kuchepusha au kuiba pembejeo zinazotolewa na Serikali kwa ajili ya wakulima.

Sauti ya 2 SACP Issa Suleima RPC Mtwara

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Korosho Tanzania, Bw. Frances Alfred, amepongeza Jeshi la Polisi kwa ushirikiano wake katika kuhakikisha usalama na uadilifu wakati wa msimu wa ugawaji wa pembejeo.

Sauti ya 1 Frances Alfred mkurugenzi wa CBT

Ameongeza kuwa uchunguzi umeanza katika Halmashauri ya Mji wa Nanyamba na maeneo mengine nayo yatafuata ili kuhakikisha kila mkulima anapata haki yake bila bugudha.

Sauti ya 1 Frances Alfred mkurugenzi wa CBT
Share:

Mwenyekiti atoa shukrani fidia ujenzi wa bandari kisiwa Mgao

 

Mwonekano wa eneo la ujenzi wa Bandari ya bidhaa chafu kabla hapajaanza maandalizi ya ujenzi hapo awali katika eneo la Kisiwa Mgao (Picha na Musa Mtepa)

Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgao ameishukuru Halmashauri ya Mtwara Vijijini kwa kulipa fidia ya ujenzi wa bandari Kisiwani Mgao, huku akitoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari za kiafya kutokana na ongezeko la wageni.

Na Musa Mtepa

 Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Mgao, kilichopo Kata ya Naumbu, Mzee Shahame, ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Vijijini kwa hatua ya kuwalipa fidia wakulima waliopisha ujenzi wa Bandari ya bidhaa chafu katika eneo la Kisiwa cha Mgao.

Akizungumza na Jamii FM Radio, Mzee Shahame amesema kuwa baada ya msuguano wa muda mrefu kati ya wananchi wa Kijiji cha Mgao, Kisiwa, na Halmashauri, hatimaye malipo ya fidia yamekamilika kwa wakulima husika. Aidha, amesema kuwa hadi sasa hakuna mwananchi yeyote kutoka kijijini kwake aliyefika kwake kulalamikia malipo hayo.

Sauti ya 1: Mzee Shahame – Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgao

Aidha, Mzee Shahame amesema kuwa ujio wa bandari hiyo umepokelewa kwa mtazamo chanya kutokana na manufaa yake kwa taifa kwa ujumla. Hata hivyo, ameeleza kuwa bado ana mashaka juu ya wananchi wa kijiji chake kunufaika moja kwa moja kwa kupata ajira za muda (vibarua) katika mradi huo.

Sauti ya 2: Mzee Shahame – Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgao

Pamoja na hayo, Mzee Shahame amesema kuwa maandalizi ya ujenzi wa bandari hiyo yameanza kuleta mabadiliko ya kiuchumi kwa wananchi, ikiwa ni pamoja na ongezeko la wageni wanaofika kijijini hapo na kupanga kwenye nyumba za wenyeji, jambo linaloongeza mzunguko wa fedha katika kijiji hicho.

Sauti ya 3: Mzee Shahame – Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgao

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo ametoa wito kwa wananchi kuchukua tahadhari za kiafya na kimazingira kutokana na ongezeko la wageni wanaoendelea kufika kijijini hapo.

Sauti ya 4: Mzee Shahame – Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgao
Share:

Mwenyekiti wa kijiji aongoza ujenzi nyumba ya mwenye ulemavu Mtwara

 

Nyumba mpya aliyojengewa mzee Zomba mlemavu wa macho kwa jitihada za mwenyekiti wa kijiji cha Mnyengedi Bi lukia Mnyachi(Picha na Musa Mtepa)

Familia ya Mzee Salumu Zomba, mwenye ulemavu wa macho, yamekabidhiwa nyumba mpya baada ya kuishi kwenye kibanda kibovu, juhudi zilizowezeshwa na viongozi wa kijiji cha Mnyengedi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Na Musa Mtepa

Baada ya kuishi katika mazingira hatarishi kwa muda mrefu, familia ya Mzee Salumu Ismail Zomba, ambaye ni mlemavu wa macho, mkazi wa Kijiji cha Mnyengedi kata ya Mkunwa mkoani Mtwara, hatimaye imekabidhiwa nyumba mpya yenye vyumba viwili na ukumbi, ikiwa ni matokeo ya juhudi za pamoja zilizoongozwa na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mnyengedi, Bi Lukia Mnyachi.

Akitoa taarifa ya ujenzi wa nyumba hiyo, Mtendaji wa Kijiji cha Mnyengedi, Bi Ebby Hamisi, amesema kuwa familia ya Mzee Zomba hapo awali ilikuwa ikiishi katika kibanda kibovu ambacho hakikutoa hifadhi ya kutosha dhidi ya mvua na jua, hali iliyowaathiri hasa watoto waliokuwa wakiishi katika mazingira hayo.

Sauti ya 1 Bi Ebby Hamisi Mtendaji wa Kijiji cha Nyengedi

Aidha, Bi Ebby ameeleza kuwa licha ya mafanikio ya ujenzi huo, familia hiyo bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali za kimaisha. Alitoa shukrani kwa wadau wote waliosaidia kufanikisha ujenzi huo, wakiwemo kituo cha redio cha Jamii FM kilichopo Naliendele, Mtwara.

Sauti ya 2 Bi Ebby Hamisi Mtendaji wa Kijiji cha Nyengedi

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Afisa Tarafa wa Mayanga, Bw. Marco Mapunda, amewapongeza wote waliojitolea katika kusaidia familia hiyo na kusema kuwa kitendo hicho ni mfano bora wa mshikamano wa kijamii na namna viongozi wanavyoweza kuwa chachu ya maendeleo kwa watu wenye uhitaji.

Sauti ya 1 Marco Mapunda afisa tarafa tarafa ya Mayanga
Marco Mapunda akizungumza na wananchi waliojitokeza kwenye kukabidhi nyumba ya Bw Zomba (Picha na Musa Mtepa)

Pia afisa tarafa ameahidi kuzibeba na kuzifanyia kazi changamoto zote zilizowasishwa kupitia risala iliyosomwa na afisa mtendaji wa Kijiji cha Nyengedi Bi Ebby Hamisi kwa kuziwasilisha katika ofisi ya mkuu wa wilaya na kuona namna ya kuisaidia familia hiyo

Sauti ya 2 Marco Mapunda afisa tarafa tarafa ya Mayanga

Kwa upande wake, Bi Lukia Mnyachi, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mnyengedi, alielezea jinsi alivyoguswa na hali ya maisha ya Mzee Zomba na kuamua kuanzisha juhudi za kutafuta msaada ili kumjengea nyumba.

Sauti ya Bi Lukia Mnyachi Mwenyekiti wa Kijiji cha Mnyengedi
Mwenyekiti wa kijiji cha Nyengedi akielezea jitihada zilizofanyika hadi kukamilika kwa ujenzi wa Nyumba ya Mzee Salumu Zomba mlemavu wa Macho na Mkazi wa kijiji cha Mnyengedi mkoani Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

Mzee Salumu Zomba, akizungumza kwa furaha, ameshukuru kwa jitihada kubwa zilizofanywa na viongozi na wadau waliomsaidia kupata makazi bora. Hata hivyo, ametumia nafasi hiyo kuomba msaada zaidi wa vitanda, magodoro, na mahitaji ya watoto wake wanaosoma.

Sauti ya Mzee Salumu Zomba mlemavu wa macho
Mzee Salumu Zomba akiwa na mke wake wakiwa katika picha ya pamoja kwenye kibanda walichokuwa wanaishi na watoto wao kabla ya Mwenyekiti wa kijiji Bi Lukia Mnyachi kufanikisha ujenzi wa Nyumba Mpya(Picha na Musa Mtepa)

Majirani wa Mzee Zomba pia wameelezea hali ngumu ya maisha anayopitia, wakisisitiza kuwa kwa kuwa ni mlemavu wa macho, anahitaji msaada wa mara kwa mara kutoka kwa jamii na serikali.

Sauti ya majirani wa Mzee Zomba
Mwonekano wa awali wa Nyumba ya Mzee Zomba kabla hajaporomoka na Mvua na kujenga kibanda kidogo cha kuishi (Picha na Musa Mtepa)
Share:

JWTZ yaadhimisha miaka 61 kwa shughuli za kijamii, michezo Mtwara

 

vikosi vya jeshi la Wananchi la Tanzania (JWTZ ) wakiwa katika maadhimisho ya siku ya kuzaliwa kwake katika viwanja vya Nangwanda Sijaona Mjini Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

JWTZ limeadhimisha miaka 61 tangu kuanzishwa kwake kwa kushiriki shughuli za kijamii ikiwemo uchangiaji damu na mpira wa kirafiki dhidi ya Jeshi la Polisi, katika viwanja vya Nangwanda Sijaona, Mtwara

Na Musa Mtepa

Jeshi la Wananchi la Tanzania (JWTZ) leo Septemba 1, 2025, limeadhimisha miaka 61 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964, kufuatia kuondoka kwa jeshi la kikoloni.

Maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya Nangwanda Sijaona mjini Mtwara, yakiongozwa na Mkuu wa Vikosi na Vikundi vya JWTZ mkoa wa Mtwara (Base Commander), Kanali James Simon Mwakinyuke.

Kanali Mwakinyuke amesema kuwa maadhimisho hayo ni kumbukizi ya kuzaliwa kwake ambapo kuelekea katika maadhimisho hayo huambatana na ufanyaji wa shughuli mbalimbali za kijamii

Sauti ya 1 Kanali James Mwakinyuke mkuu wa vikosi vya JWTZ Mtwara
Kanali James Simon Mwakinyuke akizungumza na Waandishi wa habari katika kilele cha maadhimisho ya kuzaliwa kwa JWTZ yaliyofanyika katika viwanja vya Nangwanda Sijaona mjini Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

Aidha, Kanali Mwakinyuke amesema katika kilele cha maadhimisho ya mwaka huu, Jeshi la Wananchi mkoani Mtwara limejitoa kushiriki katika zoezi la uchangiaji wa damu kupitia Mfuko wa Damu Salama – Kanda ya Kusini, pamoja na kucheza mechi ya kirafiki ya mpira wa miguu kati ya JWTZ na Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara.

Sauti ya 2 Kanali James Mwakinyuke mkuu wa vikosi vya JWTZ Mtwara
Miongoni mwaafisa wa Jeshi la Wananchi la Tanzania akiwa katika hatua za mwisho za vipimo tayari kwa kuchangia Damu katika mfuko wa taifa wa Damu Salama (Picha na Musa Mtepa)

Huu ni utaratibu wa kawaida kwa JWTZ mkoani Mtwara ambapo Mwaka jana walifanya usafi katika eneo la Mashujaa na tukachangia damu katika Zahanati ya Jeshi ya 665 Alignment.

Maadhimisho haya ni sehemu ya mwendelezo wa JWTZ kushirikiana na jamii kwa njia za kijamii na kijeshi, ikiwa ni pamoja na kudumisha amani na mshikamano ndani ya nchi.

Share:

TGNP Yakanusha tuhuma za mitandaoni kusimamia uwajibikaji na uwazi

 

Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP Bi. Gemma Akilimali

Na Mwandishi wetu

Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) umekanusha vikali tuhuma za mitandaoni kuhusu uvunjifu wa kiuongozi na matumizi mabaya ya fedha, na umesisitiza kuwa uwajibikaji na uwazi ndio nguzo kuu za kazi zake.

Mwenyekiti wa Bodi ya TGNP, Bi. Gemma S. Akilimali, alisema hatua ya kuteua Kaimu Mkurugenzi Mtendaji imefanywa kwa mujibu wa Katiba ya TGNP ya mwaka 2021, Ibara ya 19 (viii).

“Uteuzi huu ulikuwa wa lazima ili kuhakikisha mwendelezo wa taasisi wakati mchakato wa kumpata Mkurugenzi mpya ukiendelea,” alisema Akilimali.

Akizungumzia madai ya ubadhirifu, aliongeza:“Tuhuma hizi hazina msingi wowote. TGNP ina mfumo madhubuti wa usimamizi wa fedha unaokaguliwa mara kwa mara na wakaguzi wa ndani na wa nje. Tunabaki thabiti katika uwazi na uwajibikaji.”

Pia alitoa onyo kwa wanaosambaza taarifa za kupotosha:“Tutachukua hatua za kisheria chini ya Sheria ya Makosa ya Mtandao kwa yeyote anayeeneza taarifa za uongo na za kashfa. Kazi ya TGNP inaendelea bila kusimama na hatutavunjwa moyo na upotoshaji.”

Licha ya upotoshaji huo, mafanikio ya TGNP yanaonekana kupitia zaidi ya Vituo 90 vya Taarifa na Maarifa (Knowledge Centres – KCs) vilivyoanzishwa katika zaidi ya halmashauri 80 nchini. Vituo hivi vimekuwa chachu ya kupunguza umasikini, kupambana na ukatili wa kijinsia (GBV), kuongeza uelewa wa sera, na kuwaunganisha wananchi kushiriki moja kwa moja kwenye maamuzi ya maendeleo.

Amesisitiza kwamba, TGNP itaendelea kujenga uwezo kwa jamii kupitia mbinu shirikishi, na kuwajengea uwezo wananchi namna ya kuibua changamoto zao, na kuziwasilisha kwa viongozi na wafanya maamuzi ili wazifanyie kazi, lakini pia jamii ijitambue, itambue nafasi yao, na kushirikiana na uongozi ili wabadilishe mifumo kandamizi hasa ya mila na desturi na kuhakikisha rasilimali zinasogezwa karibu na wananchi kwa usawa bila ubaguzi wa kijinsia.

Bi. Akilimali alisema:“Uwajibikaji wa TGNP unadhihirika vijijini na mitaani — pale ambapo wanawake hawatembei tena kilomita nyingi kutafuta huduma za afya, pale watoto wanapopata elimu bora, na pale jamii inapopaza sauti kudai haki zao. Huo ndio ushahidi wa kweli wa TGNP.

Kwa mujibu wa Bi. Sabina Mwaliego wa Kituo cha Mshewe, Mbeya DC:“Kupitia TGNP, huduma za afya ya mama zimeimarika Mshewe. Wanawake wanajifungua salama karibu na makazi yao. Mbinu ya ‘Triple A’,  Kutathmini, Kuchambua na Kuchukua Hatua,  imetusaidia kuibua changamoto na kusukuma mabadiliko. Viongozi wetu wametuelewa na wamechukua hatua”

Afisa wa Halmashauri ya Kishapu , ambaye hakutaka kutajwa jina lake alisema: “Ushirikiano na TGNP umetusaidia kupanga bajeti kwa kuzingatia sauti za wananchi, hususan wanawake na vijana. Huduma za maji, elimu na afya zimeboreshwa kutokana na ushirikishwaji huu, Mfano kata zetu tisa zimenufaika, Ukienda Kata ya Ukenyenge, Mondo, Kishapu, Kiloleli, Songwa utaona kazi za TGNP kwenye jamii.”

Mwanachama wa TGNP, ambaye hakutaka jina lake litajwe, alisema:“Mbinu za uhamasishaji wa TGNP zinawafanya wananchi kuchukua hatua na kutumia rasilimali walizo nazo. Jamii zinakuwa na ujasiri wa kupinga ukatili na kudai mabadiliko.”

Ufanisi wa KCs umevutia hata Halmashauri ambazo hazipo moja kwa moja kwenye miradi ya TGNP. Baadhi, zikiwemo Mtwara DC, Mtwara MC, Lindi MC, Kisarawe DC, Ilala MC, Chalinze DC, Kibaha MC, Ruangwa DC na Nachingwea DC, zimeomba mwongozo kutoka TGNP ili kuanzisha KCs zao wenyewe baada ya kuona matokeo chanya kwa wenzao.

Zaidi ya kazi za ngazi ya jamii, TGNP imekuwa mshirika muhimu wa Serikali Kuu katika kusukuma mbele marekebisho ya sera na sheria zinazohusu afya, elimu na bajeti za kitaifa, kuhakikisha usawa wa kijinsia unazingatiwa katika sera zote.

Share:

Wanawake waliovunja ukimya, safari ya Coletha, Zaituni kisiasa

2 August 2025, 15:18 pm

Coletha Chiponde na Zaituni Selemani Namkola wakizungumza na Mwanaidi Kopakopa (hayupo pichani) Picha na mwandishi wetu

Na Mwanaidi Kopakopa

Walizunguka kwa miguu, walikutana na wananchi, wakahamasisha, na walipambana kwa hali na mali kuhakikisha sauti ya mwanamke inasikika katika uongozi wa ngazi ya chini

Na Mwanaidi Kopakopa

Katika miaka ya karibuni, Tanzania imeanza kushuhudia mwamko mpya wa wanawake kushiriki kikamilifu katika uongozi, hasa kwenye siasa za mitaa. Katika mazingira ambayo kwa muda mrefu yamekuwa yakitawaliwa na wanaume, wanawake sasa wanasimama kidete kudai nafasi zao za uongozi si kwa maneno tu, bali kwa vitendo.

Katika kona ya kusini mwa Tanzania, mabadiliko haya yanaanza kuchipua, si kwa baraka za kisiasa, bali kwa sauti zenye uthubutu na dhamira ya kweli kutoka kwa wanawake. Katika kata za Mkunwa na Libobe, wanawake wawili jasiri Coletha Chiponde na Zaituni Selemani Namkola waliamua kuvunja ukimya. Walichukua fomu na kujitokeza kuwania nafasi za udiwani katika kata zao. Walizunguka kwa miguu, walikutana na wananchi, wakahamasisha, na walipambana kwa hali na mali kuhakikisha sauti ya mwanamke inasikika katika uongozi wa ngazi ya chini.

Hata hivyo, licha ya jitihada kubwa walizofanya, majina yao hayakufanikiwa kupenya katika hatua ya kura za maoni. Lakini huu si mwisho wa safari. Ushiriki wao umeacha alama, umeleta majadiliano, umeibua matumaini mapya kwa wanawake na wasichana wengine katika jamii zao. Ni ushahidi wa wazi kuwa demokrasia ya kweli huanza kwa ujasiri wa mtu mmoja au wawili kusimama na kusema: “Naweza.”

Coletha na Zaituni wametoa mfano wa kuigwa. Safari yao ni mwanga kwa kizazi kijacho cha viongozi wanawake walioshikilia imani kuwa uongozi bora huanzia mtaani, kijijini, na katika vikao vya kata. Ni wajibu wa jamii sasa kuenzi jitihada hizi, kuunga mkono usawa wa kijinsia, na kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa ya kushiriki katika maamuzi yanayoathiri maisha yao ya kila siku.

Bonyeza hapa kusikiliza makala haya

Share:

Wanachama CCM Msimbati watishia kujiondoa uanachama

 

Wanachama wa CCM wakiwa katika ofisi ya chama wakipinga kuondolewa kwa jina la Rashidi Linkoni aliyeshinda kwenye kura za maoni(Picha na Musa Mtepa)

Wanachama zaidi ya 150 wa CCM Msimbati wamelalamikia kuondolewa kwa jina la Rashidi Linkoni aliyeshinda kura za maoni, wakitishia kurudisha kadi zao, huku viongozi wa wilaya wakisisitiza maamuzi ya kamati ya siasa

Na Musa Mtepa

Zaidi ya wanachama 150 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Msimbati, wilayani Mtwara Vijijini, wameonesha kutoridhishwa na kitendo cha kuondolewa jina la Rashidi Omari Linkoni, aliyeshinda kura za maoni kwa kura 116, na kurejeshwa jina la Abrehemani Hamisi aliyeshika nafasi ya pili kwa kura 101.

Wanachama hao, wakizungumza na Jamii FM Agosti 17, 2025, wamesema hatua hiyo ni dharau kwa maamuzi ya wajumbe na kutishia kurudisha kadi za chama.

Sauti ya Wanachama wa CCM Kata ya Msimbati
Baadhi ya kadi za Wanachama wa CCM wa kata ya Msimbati zilizo rejeshwa na kutupwa baada ya wanachama kutoridhishwa na kitendo cha kuenguliwa mgombea aliyepitishwa na wajumbe Kwenye kura za maoni

Mzee Musa Ali maarufu kama Mzee Chituka, muasisi wa CCM kata ya Msimbati, amesema kitendo hicho kimekwenda kinyume na maamuzi ya wajumbe na akashauri uongozi wa wilaya kufika Msimbati kufanya mazungumzo na wanachama waliomchagua Linkoni.

Sauti ya Mzee Musa Ali muasisi wa CCM kata ya Msimbati
Mzee Musa Ali muasisi wa CCM kata ya Msimbati (Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, Salumu Uchumi, mwenyekiti wa CCM tawi la Liumo, alithibitisha kuwa hadi kufikia Agosti 17, zaidi ya wanachama 150 walikuwa tayari wamerudisha kadi zao za uanachama kutokana na uamuzi huo.

Sauti ya Salumu Uchumi Mwenyekiti CCM tawi la Liumo

Rashidi Omari Linkoni, diwani mstaafu aliyeenguliwa licha ya kuongoza kura za maoni, amesema amepokea kwa namna yake maamuzi ya viongozi wa wilaya, lakini hana budi kuyakubali.

Sauti ya Rashidi Linkoni Diwani mstaafu
Rashidi Linkon aliyekuwa Diwani wa kata ya Msimbati akizungumza baada ya wanachama kuandamana wakihitaji kurejeshwa kwa jina lake lililochaguliwa kwenye kura za maoni(Picha na Musa )

Naye Shahame Masudi Ahmadi, katibu wa CCM kata ya Msimbati, amekiri jina la Abrehemani Hamisi kurudi badala ya Linkoni na kueleza kuwa ni maamuzi ya Kamati ya Siasa ya Wilaya, huku akiwataka wanachama kuwa watulivu na kufuata maelekezo ya viongozi wa juu.

Sauti ya Shame Masudi Ahmadi Katibu wa CCM kata ya Msimabti

Akizungumzia hali hiyo, Hamisi Wanyama, katibu wa siasa na uenezi CCM Mtwara Vijijini, amesema wajumbe walimteua Linkoni kwenye kura za maoni, lakini kamati ya siasa wilaya ina mamlaka ya kubadili jina endapo itaona inafaa. Aidha, ameongeza kuwa malalamiko ya wanachama ni ishara ya utovu wa nidhamu na kutoifuata itikadi ya chama.

Sauti ya 1 Hamisi Wanyama katibu wa Siasa na uenezi wilaya

Wanyama amebainisha kuwa taarifa za wanachama kurudisha kadi ameziona mitandaoni na hajapokea rasmi, lakini endapo zitafikishwa watazipokea, huku akiahidi kufika Msimbati kuzungumza na wanachama husika.

Sauti ya 2 Hamisi Wanyama katibu wa Siasa na uenezi wilaya
Katibu wa Siasa na uenezi CCM Mtwara Vijijini Hamisi Wanyama akitolea ufafanuzi juu ya malalamiko ya wanachama wa CCM kata ya Msimbati
Share:

Sikiliza jamii FM Radio

🎧 Jamii FM Live

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

Blog Archive

WAENDESHA WEBSITE

Contact Form



1 ] )[0]; $title = $recent_post['post_title']; $excerpt = wp_trim_words( $recent_post['post_content'], 20 ); $image = get_the_post_thumbnail_url( $recent_post['ID'], 'full' ); ?>