
Wakulima wa korosho Nanyamba wamelalamikia tofauti kubwa ya bei ukilinganisha na Tandahimba, hali inayowalazimisha kuhamishia mazao yao Tandahimba
Na Musa Mtepa
Baadhi ya wakulima wa zao la korosho wamehoji juu ya utofauti wa bei ya korosho unaojitokeza sokoni kati ya Halmashauri ya Nanyamba na Wilaya ya Tandahimba, hali inayosababisha wakulima kutoka Nanyamba kuhamishia mazao yao Tandahimba ili kupata bei ya juu.
Malalamiko hayo yametolewa jana, Desemba 11, 2025, wakati wa ziara ya Waziri wa Kilimo, Ndugu Daniel Chongolo, ambapo wakulima wameeleza kuwa kwa takribani miaka 10 sasa bei ya korosho imekuwa hairidhishi, sambamba na kuwepo kwa tofauti kubwa ya bei kati ya Tandahimba na Nanyamba.
Wamesema kuwa licha ya madai ya kuwepo kwa unyevu kwenye korosho zinazouzwa Nanyamba, mazao hayo hayo yakiuzwa Tandahimba hununuliwa kwa bei ya juu.
Akizungumzia changamoto zinazolikabili zao la korosho katika Halmashauri ya Nanyamba na Mkoa wa Mtwara kwa ujumla, Mbunge wa Jimbo la Nanyamba, Mhe. Abdala Chikota, amesema Serikali imeamua kujenga kongani ya viwanda vya ubanguaji wa korosho ili kuongeza thamani ya zao hilo na kupunguza changamoto za bei pamoja na changamoto nyingine zinazowakabili wakulima.

Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, amesema Nanyamba ni miongoni mwa halmashauri zinazozalisha korosho kwa wingi, hivyo ni wakati muafaka wa kuanza na kuendelea kujenga maghala makubwa yatakayosaidia kupanga na kupima viwango vya ubora wa korosho. Amesema hatua hiyo itamwezesha mnunuzi kutambua thamani ya korosho anayoenda kuinunua.

Aidha, Mhe. Chongolo amesema ili kufikia dhamira ya mwaka 2030 ya kuhakikisha korosho zinazozalishwa nchini zinabanguliwa hapa hapa nchini, ni lazima kuonesha matokeo ya ujenzi wa viwanda hivyo ili kuongeza thamani ya zao hilo.







No comments:
Post a Comment