• VIPINDI VYA ELIMU HASA KILIMO

    Tuna vipindi mbalimbali vinavyohamasisha jamii katika kilimo cha Korosho, ufuta na Mhogo. tunaendelea na jamii inafurahia uwepo wa vipindi kwa sababu wanakutana na wataalamu moja kwa moja

  • SAUTI ZA WANAJAMII HUSIKIKA

    Sauti ni muhimu hasa unapohudumia jamii ya vijijini, wasikilizaji hupenda kusikia sauti zao kwakua watu wao wanawafahamu, hivyo huwa kivutio kwako na ni rahisi jamii kuamini kuwa mpo pamoja nao

  • MICHEZO MBALIMBALI

    Afya ni sehemu ya vipindi vyetu kwenye radio, hii husaidia kuwapa fursa watu wanaopenda michezo kuwa pamoja na kubadirishana mawazo, michezo hujenga urafiki na undugu baina mwa jamii

  • WATOTO KATIKA RADIO

    Hupenda kushiriki na hujiona sehemu ya radio kwa kuwa huishi katika jamii, kipindi cha watoto kimekuwa kikifuatiliwa na watu wazima kwasababu kuu moja tu, watoto waishio vijijini huwa hawapewi kipaumbele kama tulivyofanya Jamii fm

  • SIKIKA KATIKA RADIO

    Kipengere hiki hutoa fursa kwa wanajamii wanaotuzunguka kuongea moja kwa moja na kueleza hoja zao ambazo baadae hufuatiliwa kwa undani

Mtoto ahofiwa kupoteza maisha mto mambi Mtwara

Mwonekano wa Mto Mambi unaomwaga maji Bahari ya Lindi (Likonde Namahyavi kijiji cha Ndumbwe) ukiwa umefurika maji( Picha na Musa Mtepa)

Mtoto Yasri Hamisi (14) wa kijiji cha Ndumbwe, Mtwara, anahofiwa kufariki baada ya kutumbukia mtoni alipoteleza akijaribu kugusa maji wakati akiwa na wenzake. Wananchi na vikosi vya uokoaji wanaendelea na juhudi za kumtafuta

Na Musa Mtepa

Mtoto Yasri Hamisi, mwenye umri wa miaka 14, mkazi wa kijiji cha Ndumbwe, wilaya na mkoa wa Mtwara, anahofiwa kupoteza maisha baada ya kutumbukia katika mto unaopita kijijini hapo ukitokea Bwawa la Kitere kuelekea Bahari ya Hindi upande wa Ndumbwe.

Inaelezwa kuwa Yasri aliambatana na wenzake watatu mnamo March 7, 2026 kwenda katika mto huo kwa ajili ya kufanya shughuli za uvuvi. Hata hivyo, walipofika mtoni walibadili maamuzi ya kuvua samaki na kuamua kuoga. Mmoja wao aliwaonya wenzake kuwa maji yalikuwa mengi na yana kasi hivyo yeye hangeweza kuoga.

Inadaiwa kuwa Yasri alipokuwa akijaribu kugusa maji kwa mguu ndipo alipoteleza na kutumbukia mtoni na kuzama.

Wakizungumzia tukio hilo jana, March 9, 2026, wakazi wa kijiji cha Ndumbwe wamesema wanaendelea na juhudi za kumtafuta kijana huyo kwa kufuata mwelekeo wa maji yanakoelekea kuchanganyika na maji ya Bahari ya Hindi.

Sauti ya wananchi wa kijiji cha Ndumbwe
Wananchi wa kijiji cha Ndumbwe wakiendelea na utafutaji wa Mtoto Yasri Hamisi katika eneo la Mikoko mwelekeo wa maji yanatoka Mto Mambi(Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, mwenyekiti wa kijiji cha Ndumbwe Ali Mshamu amekiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa baada ya kupata taarifa alitoa taarifa kwa wananchi wa kijiji kizima ili kuanza jitihada za kumtafuta kijana huyo. Hata hivyo hadi kufikia jana, March 9, 2026, bado hawajafanikiwa kumpata.

Sauti ya Ali Mshamu mwenyekiti wa kijiji

Akizungumzia tukio hilo, Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Ambrosi Ndunguru amesema kuwa baada ya kupokea taarifa ya tukio hilo, timu ya uokoaji ya jeshi hilo ilifika katika kijiji cha Ndumbwe na kuanza operesheni ya kumtafuta kijana huyo, lakini hadi sasa hawajafanikiwa kumpata baada ya juhudi za siku mbili huku akisema kuwa zoezi la utafutaji litaendelea kwa siku ya tatu.

Aidha, Mrakibu Ndunguru ametoa wito kwa wakazi wa eneo hilo kuepuka kusogelea mto huo kwa shughuli za uvuvi au kilimo kwa sasa, kutokana na kufurika kwa maji yenye kasi yanayotoka katika Bwawa la Kitere pamoja na vijiji vya pembezoni.

Sauti yaAmbrosi Ndunguru mrakibu msaidizi wa zimamoto
Share:

Makala: siku ya wanawake duniani 2026

 

Merina Mkuchu Meneja wa Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo SIDO Mkoa wa Mtwara (Picha na Gregory Millanzi)

Kupitia maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani (IWD), jamii inapata fursa ya kutafakari mchango, changamoto na mafanikio ya wanawake.

Gregory Millanzi na Mwanahamis Chikambu.

Katika mwanzo wa historia ya mwanadamu, kabla ya ustaarabu kujengeka na kabla jamii haijaweka mifumo ya maisha tunayoijua leo, kulikuwepo mwanamke. Mwanamke ndiye aliyebeba tumaini la uhai, mlezi wa kizazi na nguzo ya familia. Kupitia mikono yake jamii imekua, kupitia hekima yake maadili yamefundishwa, na kupitia uvumilivu wake maisha yameendelea. Tangu zamani, uwepo wa mwanamke umeendelea kuwa msingi muhimu katika kujenga na kuendeleza maisha ya binadamu.

Kwa mwaka huu, maadhimisho yamebeba kauli mbiu “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050.

Katika kila zama, mwanamke amekuwa kama mwanga unaoangaza njia ya maisha ya binadamu. Akiwa mama, mlezi, mwalimu na wakati mwingine kiongozi wa kimya kimya ndani ya jamii, mchango wake umeendelea kuandika sura muhimu katika historia ya maendeleo ya dunia. Ni nguvu ambayo mara nyingi haionekani wazi kwa macho, lakini athari yake imekuwa kubwa katika kujenga kizazi, kuimarisha familia na kusimika misingi imara ya jamii.

Debora Didi afisa ustawi wa Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara (picha na Gregory Millanzi)

Hata hivyo, kwa miaka mingi wanawake na wasichana wamekumbana na changamoto na vikwazo mbalimbali katika nyanja tofauti za maisha. Baadhi walinyimwa fursa sawa za kupata elimu, wengine hawakupewa nafasi katika uongozi, na wengi hawakushirikishwa kikamilifu katika maamuzi muhimu yanayoathiri maisha ya jamii. Hali hii ilisababisha sauti ya mwanamke kutosikika ipasavyo licha ya mchango mkubwa aliokuwa akiutoa kila siku katika maendeleo ya familia na taifa.

Licha ya changamoto hizo, dunia inaendelea kubadilika. Leo hii, sauti ya mwanamke inazidi kusikika na nafasi yake katika jamii inaendelea kutambuliwa. Kupitia maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani (IWD), jamii inapata fursa ya kutafakari mchango, changamoto na mafanikio ya wanawake. Kwa mwaka huu, maadhimisho yamebeba kauli mbiu “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi Kufikia Dira 2050.” Makala haya yameandaliwa na Gregory Millanzi akishirikiana na Mwanahamis Chikambu.

Ili kusikia makala haya, bonyeza hapa

Share:

Wananchi waomba kuharakishwa fidia ya utafiti wa Mafuta na Gesi asilia Lindi na Mtwara

 

Baadhi ya mitambo iliyokuwa inatumika katika kufanyia utafiti wa Gesi asilia na Mafuta katika kitalu cha Lindi na Mtwara ikiwa imepaki (Picha na Musa Mtepa)

Wananchi katika vijiji vya Lindi na Mtwara walalamikia kuchelewa kulipwa fidia ya mazao yaliyoharibiwa wakati wa utafiti wa mafuta na gesi, huku TPDC ikisema tathmini imefikia asilimia 51 na malipo yanatarajiwa kuanza

Na Musa Mtepa

Wananchi wanaoishi katika vijiji vilivyopitiwa na mradi wa utafiti wa gesi na mafuta katika wilaya za Lindi na Mtwara wamelalamikia kuchelewa kulipwa fidia ya mazao yao yaliyoharibiwa wakati wa kuweka njia za kupita mitambo ya utafiti.

Wananchi hao wamesema kuwa utafiti wa mafuta na gesi ni jambo muhimu kwa uchumi na maendeleo ya taifa, lakini wanashangazwa na kuchukua muda mrefu kulipwa fidia ya mazao yao yaliyoondolewa wakati wa shughuli za utafiti huo.

Akizungumza Febraury 28,2026  Hamza Karimu Mrope, mwenyekiti wa kitongoji cha Likuluwilo katika kijiji cha Hiari, wilayani Mtwara, amesema jamii inashukuru kwa uwepo wa utafiti huo lakini wananchi wanashangaa kwa nini fidia ya mazao yao yaliyoondolewa wakati wa utafiti imechukua muda mrefu kulipwa.

Sauti ya Hamza Karimu Mwenyekiti wa kitongoji

Kwa upande wake, Mohamedi Mbaki ambaye ni Diwani wa Kata ya Mayanga amesema ni kweli kuwa hadi sasa wananchi hawajalipwa fidia hiyo. Amesema ni muhimu kwa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) kuhakikisha fedha za fidia zinalipwa kwa wakati ili wananchi wanufaike na mazao yao yaliyotolewa wakati wa utafiti wa mafuta na gesi katika mashamba yao.

Sauti ya Mohamedi Mbaki Diwani kata ya Mayanga

Akitoa ufafanuzi kuhusu malalamiko hayo, Mjiolojia na Meneja wa Mradi wa Utafiti wa Mafuta na Gesi Asilia kupitia kitalu cha Lindi/Mtwara, Dkt Shaidu Nuru, amesema zoezi la tathmini ya fidia katika mradi huo wenye ukubwa wa kilometa za mraba 736.3 limekamilika kwa asilimia 51, na hatua iliyobaki ni malipo ya fidia.

Amesema utaratibu uliopo sasa ni kuandaa vitabu vitakavyowasilishwa kwa maafisa mbalimbali kwa ajili ya kukamilisha mchakato wa malipo, na zoezi hilo tayari limekamilika.

Aidha, Dkt Nuru amesema jumla ya shilingi milioni 477.9 zimeidhinishwa na Mthamini Mkuu kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi 2,571 walioathiriwa na mradi huo. Ameongeza kuwa awali walikuwa wamepanga ifikapo mwezi Februari 2026 wawe tayari wameanza kulipa fidia hiyo.

Share:

Waziri wa Nishati ahimiza ushirikiano miradi ya CSR Mtwara

 

Power Plant ya kijiji cha Hiari ambapo Waziri wa Nishati Mhe. Deogratius Ndejembi katika ziara yake alipata nafasi ya kutembelea na kujionea utendaji kazi wake(Picha na Musa Mtepa)

Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, ahimiza ushirikiano wa TPDC na viongozi wa Mtwara katika miradi ya CSR, huku akisisitiza ajira na uwezeshaji wa wananchi kwenye miradi ya gesi asilia

Na Musa Mtepa

Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, ameliagiza Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) pamoja na kampuni zinazojihusisha na shughuli za gesi asilia mkoani Mtwara kushirikiana kwa karibu na viongozi wa maeneo husika wakati wa utekelezaji wa miradi ya Uwajibikaji kwa Jamii (CSR).

Ameyasema hayo Februari 27 na 28, 2026 alipokuwa katika ziara ya kikazi, akisisitiza umuhimu wa kushirikiana na viongozi wa vijiji, madiwani, wabunge na halmashauri ili miradi inayotekelezwa iendane na gharama halisi pamoja na thamani ya fedha inayowekezwa na Serikali.

Sauti ya Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati

Aidha, Mhe. Ndejembi ameagiza kuendelezwa kwa uwezo wa Watanzania, hususan wa maeneo yanayozunguka miradi ya gesi, ili waweze kushiriki kikamilifu katika utoaji wa huduma hatua hiyo inayolenga kuongeza mzunguko wa fedha na kukuza uchumi wa maeneo husika.

Sauti ya Deogratius Ndejembi Waziri wa Nishati

Akizungumzia utekelezaji wa miradi ya CSR, Mjiolojia Mwandamizi ambaye pia ni Meneja wa Mradi wa Utafutaji wa Mafuta na Gesi katika Kitalu cha Lindi–Mtwara, Shaidu Nuru, amesema kuwa wakati wa utekelezaji wa mradi huo wamefanikiwa kurejesha faida kwa jamii kupitia miradi mbalimbali.

Ametaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni pamoja na ununuzi wa mabati kwa ajili ya Soko la Kijiji cha Mkwajuni Juu, ujenzi na ukarabati wa viwanja vya shule, uboreshaji wa barabara za kuunganisha vijiji, pamoja na kusaidia sekta ya afya katika maeneo yanayozunguka mradi.

Sauti ya Shaidu Nuru Meneja Mradi wa Utafutaji wa Gesi na Mafuta Kitalu cha Lindi–Mtwara

Shaidu Nuru amesema lengo kuu la mradi wa Lindi –Mtwara ni kutafuta rasilimali za mafuta na gesi asilia ili kuhakikisha taifa linakuwa na nishati ya kutosha, hatua itakayochochea maendeleo kuanzia ngazi ya kijiji hadi taifa kwa ujumla.

Ameongeza kuwa mbali na manufaa ya moja kwa moja yatokanayo na upatikanaji wa nishati, pia kuna fursa mbalimbali kwa jamii zinazoguswa na mradi huo, ikiwemo ajira. Amesema waliendesha kampeni maalum kuhakikisha kazi zote zisizohitaji utaalamu wa hali ya juu zinafanywa na wakazi wa maeneo husika, kama ilivyotekelezwa wakati wa mradi huo.

Sauti ya Shaidu Nuru Meneja Mradi wa Utafutaji wa Gesi na Mafuta Kitalu cha Lindi–Mtwara

Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini, Mhe. Arif Premji, ameipongeza Serikali kwa kuendelea kutekeleza miradi mikubwa ya gesi asilia mkoani Mtwara huku akibainisha kuwa miradi hiyo pamoja na ile ya CSR imekuwa na mchango mkubwa katika kuboresha huduma za kijamii na maendeleo ya wananchi wa eneo hilo.

Sauti ya Arif Premji Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini

Share:

TAKUKURU Mtwara yadhibiti Milioni 15.3 za makato ya Korosho na ufuta

 

Kaimu mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mtwara Mwanakombo Rajabu akitoa taarifa za mafanikio ya utendaji kazi kwa kipindi cha Mwezi Oktoba hadi Disemba mwaka 2025 (Picha na Musa Mtepa)

TAKUKURU Mkoa wa Mtwara Region imedhibiti zaidi ya shilingi milioni 15.3 za makato ya korosho na ufuta, kupokea malalamiko 53 ya rushwa, na kusimamia marekebisho ya miradi ya maendeleo yenye thamani ya zaidi ya shilingi bilioni 2.03

Na Musa Mtepa

Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa  (TAKUKURU) mkoa wa Mtwara imesaidia kurejesha na kudhibiti fedha zilizotokana na makato ya mauzo ya korosho na ufuta katika halmashauri tatu kati ya tisa zilizopo mkoani humu.

Akitoa taarifa ya mafanikio ya utendaji kazi wa TAKUKURU Mkoa wa Mtwara kwa kipindi cha Oktoba hadi Disemba 2025 kwa waandishi wa habari, Machi 3, 2026, Kaimu Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa Mtwara, Mwanakombo Rajabu, amesema kuwa zaidi ya shilingi milioni 15.3 zimedhibitiwa na kati ya fedha hizo, shilingi 11,896,000.00 zimerejeshwa katika Halmashauri ya Masasi, shilingi 2,571,500.00 Halmashauri ya Tandahimba, na shilingi 861,000.00 katika Halmashauri ya Newala.

Sauti ya Mwanakombo Rajabu Kaimu mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mtwara

Aidha, katika ufuatiliaji wa matumizi ya fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Bi. Mwanakombo amesema TAKUKURU ilitoa mapendekezo ya kurekebisha mapungufu katika miradi minane yenye thamani ya jumla ya shilingi 2,035,825,000/=na kuelezea  kuwa mapungufu hayo yamerekebishwa kikamilifu baada ya taasisi hiyo kutembelea tena miradi husika kwa ajili ya uhakiki.

Sauti ya Mwanakombo Rajabu Kaimu mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mtwara

Akizungumzia masuala ya uchunguzi na mashitaka kwa kipindi cha Mwezi Oktoba hadi Disemba pamoja na mikakati ya Januari hadi Machi, Bi. Mwanakombo amesema jumla ya malalamiko 53 yamepokelewa, ambapo 33 kati yake yanahusu tuhuma za rushwa na kubainisha kuwa uchunguzi wa malalamiko hayo unaendelea katika hatua mbalimbali.

Sauti ya Mwanakombo Rajabu kaimu mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mtwara

Bi. Mwanakombo Rajabu ametumia nafasi hiyo kutoa wito kwa wananchi kutoa taarifa za vitendo vya rushwa na kushiriki kikamilifu katika ufuatiliaji wa miradi ya serikali inayotekelezwa mkoani Mtwara, ikiwemo ujenzi wa stendi mpya ya mabasi ya Mkanaledi.

Sauti ya Mwanakombo Rajabu kaimu mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Mtwara
Share:

CRDB Foundation na serikali yawawezesha vijana Mtwara

 

Pikipiki,Guta na Bajaji zilikabidhiwa March 2,2026 na waziri wa vijana Dkt Joel Nanauka kwa vijana 25 mkoani Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

CRDB Bank Foundation imekabidhi Pikipiki, Bajaji na Guta zenye thamani ya shilingi milioni 140 kwa vijana wa Mtwara, kuendeleza mikopo nafuu kwa ushirikiano na Wizara ya Maendeleo ya Vijana

Na Musa Mtepa

Benki ya CRDB kupitia CRDB Bank Foundation kwa kushirikiana na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, imekabidhi Pikipiki, Bajaji na Guta mkoani Mtwara ikiwa ni sehemu ya mwendelezo wa mikopo inayotolewa kwa kushirikiana na wizara hiyo kwa vijana wa Kitanzania.

Akizungumza kuhusu mikopo hiyo Machi 2, 2026, Meneja Mwandamizi wa CRDB Bank Foundation anayesimamia mikopo yenye masharti nafuu ambaye pia ni msimamizi wa uhusiano na ubia na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali, Baraka Kiyaro, amesema wamekabidhi Bajaji 5, Guta 5 na Pikipiki 15 zenye thamani ya shilingi milioni 140 kama sehemu ya mwendelezo wa mikopo inayotolewa kwa kushirikiana na Wizara ya Vijana.

Sauti ya Baraka Kiyaro Mwandamizi CRDB benk Foundation

Pamoja na hayo, Baraka Kiyaro amesema pia wameingia makubaliano na wizara mbalimbali kwa lengo la kuwawezesha vijana, wanawake na watu wenye mahitaji maalumu nchini. Amesema wanawasaidia kwa kuwajengea uwezo kupitia elimu ya fedha, kuwapatia mafunzo ya ujasiriamali pamoja na kuwatafutia masoko ili kuwaondoa kwenye mikopo chechefu maarufu kama “kausha damu”.

Sauti ya Baraka Kiyaro Mwandamizi CRDB benk Foundation

Aidha, Baraka amesema kumekuwa na mwitikio mkubwa wa vijana kujitokeza kupata mikopo hiyo, hali inayoonesha kuheshimu na kufurahia jitihada zinazofanywa na Serikali kwa ajili ya vijana.

Sauti ya Baraka Kiyaro Mwandamizi CRDB benk Foundation

Naye meneja  CRDB kanda ya kusini, Emmanuel Biganio, amesema tangu kuanzishwa kwa CRDB Foundation mwaka 2023, imeweza kuwafikia vijana laki saba na ishirini (720,000), huku zaidi ya shilingi bilioni 20.1 zikitolewa kama mikopo na mitaji wezeshi. Amesema makubaliano na wizara ni kuongeza kasi zaidi katika utekelezaji wa malengo yaliyowekwa na Wizara ya Vijana.

Sauti ya Emmanuel Biganio meneja wa CRDB kanda ya kusini.

Mikopo hiyo imetolewa Machi 2, 2026 na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Vijana (Vijana Platform) mkoa wa Mtwara uliofanyika katika Chuo cha Stella Maris Mtwara, ambapo zaidi ya vijana 25 wamenufaika na mikopo hiyo.

Share:

Vijana 25 Mtwara wapokea mikopo ya serikali

 

Baadhi ya pikipiki zilizotolewa kwa mkopo wa masharti nafuu kwa vijana 25 mkoani Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

Zaidi ya vijana 25 Mtwara wamenufaika na mikopo nafuu, wakiwemo wapokeaji wa pikipiki, bajaji na guta, iliyokabidhiwa na Waziri wa Vijana kwa lengo la kukuza biashara na ajira

Na Musa Mtepa

Vijana 25 mkoani Mtwara wamenufaika na mikopo yenye masharti nafuu inayosimamiwa na Wizara ya Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana. Mikopo hiyo imetolewa leo, March 2, 2026, na Waziri wa Vijana, Joel Nanauka, baada ya kuzinduliwa kwa jukwaa la Vijana (Vijana Platform) mkoani Mtwara.

Waziri Nanauka amesema kuwa amewakabidhi vijana pikpiki 15, bajaji 5 na guta 5 vyenye thamani ya jumla ya Shilingi milioni 140, vyote ikiwa na bima zao, huku wakipewa muda wa miezi mitatu kuanza kulipa marejesho.

Sauti ya Dkt. Joel Nanauka, Waziri wa Vijana

Akizungumza kwa niaba ya mkoa, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Dolnad Msengi, amewashauri vijana kuchangamkia fursa hiyo na kuachana na hoja za masharti magumu ya mikopo, huku akiunga mkono jitihada za Rais wa nchi katika kuwasaidia vijana kupata uchumi.

Sauti ya Dolnad Msengi, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara

Katibu wa chama cha waendesha boda boda na bajaji mkoa wa Mtwara, Mshamu Ali, amesema kuwa hatua ya serikali kukopesha chombo baada ya fedha italeta tija kubwa kwa vijana ikilinganishwa na ukopeshaji wa fedha pekee.

Sauti ya Mshamu Ali, Katibu wa Dereva Boda Boda na Bajaji Mtwara

Vijana wanufaika wamesema wanashukuru kwa jitihada za serikali na kueleza kuwa mikopo hiyo itawasaidia kusogeza mbele maendeleo yao binafsi na ya taifa kwa ujumla.

Sauti ya vijana wanufaika na mikopo ya vijana
Share:

Sikiliza jamii FM Radio

🎧 Jamii FM Live

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

Blog Archive

WAENDESHA WEBSITE

Contact Form



1 ] )[0]; $title = $recent_post['post_title']; $excerpt = wp_trim_words( $recent_post['post_content'], 20 ); $image = get_the_post_thumbnail_url( $recent_post['ID'], 'full' ); ?>