
Mzee Salumu Somba mkazi wa Mnyengedi, Mtwara, mlemavu wa macho, anaomba msaada wa makazi, mavazi, na mahitaji ya msingi kwa ajili ya familia yake kutokana na hali ngumu ya maisha.
Na Musa Mtepa
Mzee Salumu Somba, mkazi wa Kijiji cha Mnyengedi kata ya Mkunwa katika Halmashauri ya Mtwara Vijijini, anaomba msaada kutoka kwa wadau na wasamaria wema ili apate makazi bora na mahitaji ya msingi ya kibinadamu.
Mzee Somba ni mlemavu wa macho ambaye anaeleza kuwa maisha anayopitia kwa sasa ni magumu mno kutokana na hali yake ya ulemavu, ukosefu wa makazi bora, mavazi na upatikanaji wa chakula cha uhakika kwa familia yake.
Mzee huyo mwenye mke mmoja na watoto wawili wanaosoma darasa la kwanza na la tatu, anasema kwa sasa nyumba yake imeharibika kiasi kwamba wakati wa mvua hunyeshewa akiwa ndani na familia yake, hali inayowaweka kwenye mazingira hatarishi kiafya na kimaisha.

Mwenyekiti wa Kijiji cha Mnyengedi, Bi Lukia Mnyachi, amesema alifahamishwa kuhusu hali ya Mzee Somba na mwanakijiji mmoja. Baada ya kutembelea eneo analoishi mzee huyo na kujionea mazingira halisi, aliamua kuanzisha jitihada za kumsaidia.
Aidha Bi Lukia amesema baada ya kupata mchango kutoka kwa umoja wa wenyeviti akaanza mchakato rasmi wa kujenga nyumba kwa ajili ya Mzee Somba kwa kuendelea kushirikisha viongozi wengine wa juu ambao kwa namna moja au nyingine wameendelea kumuunga mkono katika kulifanikisha hilo.
Licha ya hatua hizo, bado kuna uhitaji mkubwa wa msaada zaidi kwa familia hiyo — hasa vifaa vya msingi kama kitanda, magodoro, mashuka na mavazi kwa watoto wake.
Baadhi ya wakazi wa kijiji hicho wamejitokeza kwa moyo mmoja kushiriki katika jitihada za kumjengea Mzee Somba banda la muda, huku wakiendelea kuomba msaada zaidi kutoka kwa wadau wa maendeleo na mashirika ya kijamii.

Kwa wale wanaotaka kuchangia au kumsaidia Mzee Somba na familia yake, wanaombwa kuwasiliana na uongozi wa Kijiji cha Mnyengedi au kupitia kituo cha Jamii FM Radio kwa maelekezo zaidi.










