
Nyumba ya mkazi wa Mangamba Chini, Bw. Roboti, imeteketea kwa moto asubuhi ya Oktoba 8, 2025, kutokana na mkaa uliokuwa bado una moto. Jeshi la Zimamoto lilifika kwa haraka kuzima moto huo, huku viongozi na majirani wakitoa pole na elimu ya tahadhari dhidi ya moto majumbani
Na Grace Khamisi
Mkazi mmoja wa mtaa wa Mangamba Chini, katika Manispaa ya Mtwara Mikindani, anayefahamika kwa jina la Roboti, amejikuta katika wakati mgumu baada ya nyumba yake kuteketea kwa moto. Tukio hilo limetokea majira ya saa tatu asubuhi, Oktoba 8, 2025.
Wakizungumza na Jamii fm redio, majirani wa Bw. Roboti, Bi. Mariamu Yusufu na Mohamedi Moa ,wamesema kuwa wakati moto huo ulipoanza walikuwa nyumba ya jirani, karibu na nyumba ya Roboti, ndipo walipoona moshi na kuwajulisha majirani wengine ili kusaidia kuzima moto huo.
Kwa upande wake, Bw. Roboti ambaye ni muathirika wa tukio hilo, amesema kuwa alipata taarifa za kuungua kwa nyumba yake kupitia simu alipokuwa kazini, na alilazimika kukatisha kazi ili kufika nyumbani haraka kwa ajili ya kuokoa mali na kusaidia kuuzima moto huo.
Naye Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mtwara, Ambros Ndunguru, amesema chanzo cha moto huo ni kiroba cha mkaa kilichowekwa na Bw. Roboti bila kuchunguza kama mkaa huo ulikuwa bado una moto.
Aidha, Mrakibu Ndunguru ametumia fursa hiyo kutoa elimu kwa wananchi juu ya matumizi sahihi ya majiko ya mkaa, huku akitoa onyo dhidi ya tabia ya kuzima mkaa wa moto kwa kutumia majivu, akisema ni hatari kwa usalama wa makazi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Mtaa wa Mangamba Chini, Bw. Abdala Abdala, amempa pole Bw. Roboti kwa tukio hilo, huku akilishukuru Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kufika kwa haraka na kuzuia madhara makubwa zaidi.






No comments:
Post a Comment