
Mgombea urais wa CUF, Gombo Samandito Gombo, amewataka Watanzania kujitokeza kwa wingi kupiga kura Oktoba 29, 2025, akiahidi huduma bora za jamii na maendeleo ya kweli endapo chama chake kitaunda serikali
Na Musa Mtepa
Mgombea urais kupitia tiketi ya Chama cha Wananchi (CUF), Gombo Samandito Gombo, amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, 2025, kwa kuchagua viongozi wanaowataka ili kuleta maendeleo ya kweli kwa taifa.
Akizungumza na Waandishi wa habari Oktoba 8, 2025, mjini Mtwara, Gombo amesema kuwa fikra za baadhi ya wananchi kutoshiriki kupiga kura haziwezi kuwasaidia Watanzania kwa namna yoyote ile na kusisitiza kuwa ni muhimu kila mmoja kutumia haki na nguvu yake ya kikatiba kwa kumpigia kura mgombea wa CUF.
Aidha, Gombo ameongeza kuwa chama hicho hakikatishwi tamaa na idadi ya watu wanaojitokeza kwenye mikutano ya kampeni, kwani CUF inaamini kuwa uungwaji mkono kutoka kwa wananchi ni mkubwa na unaendelea kuimarika kila siku.
Akizungumzia sera za chama chake, Gombo amesema kuwa endapo CUF itashinda uchaguzi na kuunda serikali, itahakikisha wananchi wa Mtwara na Watanzania kwa ujumla wanapata huduma bora za kijamii, ikiwemo matibabu bure na miundombinu ya kisasa.
Chama cha Wananchi (CUF) ni miongoni mwa vyama vinavyowania nafasi ya kuongoza nchi katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ambapo wagombea mbalimbali wameendelea na kampeni zao katika maeneo mbalimbali nchini.







No comments:
Post a Comment