• VIPINDI VYA ELIMU HASA KILIMO

    Tuna vipindi mbalimbali vinavyohamasisha jamii katika kilimo cha Korosho, ufuta na Mhogo. tunaendelea na jamii inafurahia uwepo wa vipindi kwa sababu wanakutana na wataalamu moja kwa moja

  • SAUTI ZA WANAJAMII HUSIKIKA

    Sauti ni muhimu hasa unapohudumia jamii ya vijijini, wasikilizaji hupenda kusikia sauti zao kwakua watu wao wanawafahamu, hivyo huwa kivutio kwako na ni rahisi jamii kuamini kuwa mpo pamoja nao

  • MICHEZO MBALIMBALI

    Afya ni sehemu ya vipindi vyetu kwenye radio, hii husaidia kuwapa fursa watu wanaopenda michezo kuwa pamoja na kubadirishana mawazo, michezo hujenga urafiki na undugu baina mwa jamii

  • WATOTO KATIKA RADIO

    Hupenda kushiriki na hujiona sehemu ya radio kwa kuwa huishi katika jamii, kipindi cha watoto kimekuwa kikifuatiliwa na watu wazima kwasababu kuu moja tu, watoto waishio vijijini huwa hawapewi kipaumbele kama tulivyofanya Jamii fm

  • SIKIKA KATIKA RADIO

    Kipengere hiki hutoa fursa kwa wanajamii wanaotuzunguka kuongea moja kwa moja na kueleza hoja zao ambazo baadae hufuatiliwa kwa undani

Mashamba 15 yashambuliwa na viboko Mnuyo

 

Sehemu ya mashamba ya wakulima wa kijiji cha Mnuyo kata ya Msimbati yaliyoshambuliwa na Viboko (Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa kijiji cha Mnuyo mkoani Mtwara wamelalamikia mashambulizi ya viboko mashambani, wakiiomba serikali kuchukua hatua za haraka kuwalinda na kuzuia hatari ya baa la njaa.

Na Musa Mtepa

Wananchi wa Kijiji cha Mnuyo, kata ya Msimbati, Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara, mkoani Mtwara, wameiomba serikali kupitia mamlaka zinazohusika na wanyamapori kufika kijijini hapo ili kuwaondolea changamoto ya wanyama aina ya viboko wanaoshambulia mashamba yao ya mpunga.

Wakizungumza na Jamii FM Redio Aprili 10,2026, wananchi hao wamesema kuwa katika siku za hivi karibuni wamekuwa wakikumbwa na changamoto kubwa ya viboko kuvamia mashamba yao ya mpunga nyakati za usiku, hali inayowatishia baa la njaa siku za usoni.

Sauti ya wakulima wa mpunga Kijiji cha Mnuyo

Aidha, wananchi hao wameiomba serikali kuwasaidia kwa haraka kutatua changamoto hiyo, ambayo imekuwa kubwa kwao kiasi cha baadhi yao kukata tamaa ya kuendelea na shughuli za kilimo kutokana na uwepo wa wanyama hao.

Sauti ya wakulima wa mpunga Kijiji cha Mnuyo
Kinyesi cha Mnyama Boko kikionekana pembezoni mwa shamba la Mpunga (Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, mwenyekiti wa Kijiji cha Mnuyo, Yusuf Salumu, amekiri kupokea taarifa za uwepo wa wanyama hao katika eneo hilo, akisema tayari amezifikisha katika Halmashauri ya Wilaya kwa ajili ya hatua zaidi.

Aidha, mwenyekiti huyo amesema viboko hao wanaotoka Mto Ruvuma wameshashambulia mashamba 15 ya wakulima wa kijiji hicho, huku akiomba mamlaka zinazohusika na wanyamapori kuchukua hatua za haraka kuwaondoa wanyama hao.

Sauti ya Yusuf Salumu, mwenyekiti wa Kijiji cha Mnuyo
Share:

Manispaa ya Mtwara Mikindani yaimarisha ulinzi wa mtoto

 

Fatu Mapua, Afisa Ustawi wa Jamii Manispaa ya Mtwara Mikindani akiongoza mdahalo wa wadau juu ya ulinzi na usalama wa mtoto uliofanyika Aprili 11,2026 katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri. (Picha na Musa Mtepa)

Jamii imetakiwa kushiriki kikamilifu kulinda watoto dhidi ya ukatili, kupitia elimu na ushirikiano wa . wadau mbalimbali, ili kuhakikisha usalama wa watoto chini ya miaka 18 katika Manispaa ya Mtwara Mikindani

Na Musa Mtepa

Jamii imeaswa kila mmoja kusimama katika nafasi yake ili kuhakikisha usalama na ulinzi wa mtoto vinakuwa kipaumbele, kwa lengo la kumuweka salama dhidi ya vitendo vya ukatili na matukio hatarishi.

Wito huo umetolewa Aprili 11, 2026, katika mdahalo uliowakutanisha wadau mbalimbali, wakiwemo mawakala wa magari ya abiria, madereva wa bodaboda, washereheshaji wa sherehe (MC), ma-DJ na waandishi wa habari.

Mdahalo huo ulioandaliwa na Idara ya Ustawi wa Jamii ya Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, ulikuwa na lengo la kupunguza na hatimaye kutokomeza vitendo vya ukatili dhidi ya watoto wenye umri chini ya miaka 18 katika manispaa hiyo.

Wakizungumza katika mdahalo huo, washiriki wameipongeza halmashauri kwa kuandaa mdahalo huo, wakisema umewawezesha kupata maarifa muhimu ambayo wataenda kuyafanyia kazi katika shughuli zao za kila siku.

Aidha, wamesema mbali na kuwa sehemu ya kutoa elimu kwa jamii kuhusu matukio hatarishi kwa watoto, wametoa wito kwa halmashauri kupitia viongozi wa mitaa kuendelea kutoa elimu kuhusu ulinzi wa watoto pamoja na vihatarishi vinavyochangia ukatili huo, ikiwemo watoto kuhusishwa katika matukio ya usiku, kuhudhuria kumbi za starehe na kushiriki shughuli za mitaani.

Sauti ya wajumbe walioshiriki katika mdahalo

Akizungumzia tuhuma za baadhi ya madereva wa bodaboda kuhusishwa na matukio ya ukatili kwa watoto, Hance Bruno, dereva bodaboda kutoka kata ya Shangani, amekiri kuwepo kwa baadhi yao wenye tabia hiyo, huku akiahidi kwenda kulifanyia kazi suala hilo katika kituo chake. Pia ametoa wito kwa wazazi kuwa makini na watoto wao, hasa katika kipindi cha sikukuu.

Sauti ya Hance Bruno Dereva bodaboda kata ya Shangani

Kwa upande wake, Fatu Issa Mapua, Afisa Ustawi wa Jamii wa Manispaa ya Mtwara Mikindani, amesema miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa ni pamoja na matukio ya ukatili yaliyojitokeza ndani ya manispaa hiyo na kupanga mikakati ya baadaye ili kuwasaidia watoto kuwa salama katika maeneo yao.

Sauti ya Fatu Issa Mapua afisa ustawi Manispaa ya Mtwara Mikindani

Aidha, Bi. Mapua amesema matukio ya ukatili bado yapo katika Manispaa ya Mtwara Mikindani, ndiyo maana wamekuwa wakikutana na makundi mbalimbali ili kuwapatia elimu na kuiwezesha jamii kutoa taarifa pale matukio yanapotokea. Ameongeza kwa kutoa wito kwa wananchi kwamba usalama na ulinzi wa mtoto ni jukumu la kila mmoja.

Sauti ya Fatu Issa Mapua afisa ustawi wa Jamii Manispaa ya Mtwara Mikindani
Share:

Makato ya korosho kikwazo mradi wa soko Mnyahi

 

Mwonekano wa soko la zamani la kijiji cha Mnyahi kata ya Milangominne halmashauri ya mji Nanyamba mkoani Mtwara ambalo wakulima wa zao la korosho wanakatwa shilingi 20 kwa kila kilo moja inayouzwa ili fedha ijenge soko jipya (Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa Mnyahi Mtwara walalamikia kuchelewa kwa ujenzi wa soko licha ya makato ya korosho, wakitupia lawama viongozi wa kijiji na mfumo wa ukusanyaji fedha.

Na Musa Mtepa

Wananchi wa kijiji cha Mnyahi, kata ya Milangominne mkoani Mtwara, wameulalamikia uongozi wa kijiji pamoja na Halmashauri ya Mji Nanyamba kwa kuwa kikwazo cha kutokamilika kwa miradi ya maendeleo inayoanzishwa na kijiji hicho, inayotegemea makato ya zao la korosho linalolimwa katika eneo hilo.

Wakizungumza na Jamii FM Radio, wananchi hao wamesema kuwa takribani miaka mitatu sasa imepita tangu walipokubaliana katika mkutano wa kijiji kukatwa shilingi 20 kwa kila kilo moja ya korosho, ili fedha zitakazopatikana ziweze kuwezesha ujenzi wa soko jipya kijijini hapo.

Sauti ya wananchi wa kijiji cha Mnyahi

Aidha, wananchi hao wamesema kuwa changamoto inayosababisha kuchelewa kwa ujenzi wa soko hilo ipo katika serikali ya kijiji, wakidai kuwa baadhi ya viongozi hawawajibiki ipasavyo, hususan katika uendeshaji wa mikutano ya kijiji. Pia wameomba viongozi wakuu wa vyama vinavyowaweka madarakani viongozi wa vijiji kuwafuatilia kwa karibu utendaji wao wa kazi baada ya uchaguzi.

Sauti ya 2 wananchi wa kijiji cha Mnyahi

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji cha Mnyahi, Hamisi Salumu Mpangu, amesema kuwa changamoto kubwa ya upatikanaji wa fedha hizo kwa wakati na utekelezaji wa miradi ya maendeleo inatokana na matatizo anayokutana nayo mtendaji wa kijiji katika kutumia mfumo wa NeST, hali inayochangiwa na umri pamoja na uelewa mdogo wa matumizi ya mfumo huo.

Sauti ya Hamisi Salumu Mpangu, Mwenyekiti wa kijiji cha Mnyahi
Mwenyekiti wa kijiji cha Mnyahi Bw Hamisi Salumu Mpangu akitolea maelezo juu ya malalamiko ya wananchi wa kijiji hicho(Picha na Musa Mtepa)

Akitolea ufafanuzi juu ya malalamiko ya wananchi wa kijiji cha Mnyahi, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Nanyamba, Mhe. Hassani Ali Mauji, amesema kuwa fedha hizo hukusanywa awali na MAMCU, na baada ya msimu kumalizika hufanya makusanyo ya pamoja ya halmashauri yote na kuziingiza katika akaunti ya halmashauri. Baadaye, mkurugenzi huzipeleka katika akaunti za vijiji kulingana na kiwango cha fedha kilichokusanywa.

Aidha, amesema kuwa ili viongozi wa kijiji waweze kutoa fedha hizo, ni lazima kuwepo na muhtasari wa vikao vya mikutano ya kijiji unaoeleza matumizi ya fedha hizo katika miradi ya maendeleo ya wananchi. Ameongeza kuwa jukumu la ufuatiliaji wa taratibu hizo ni la mtendaji wa kijiji husika.

Sauti ya Hassani Ali Mauji, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Nanyamba

Share:

Wananchi walia na uchakavu wa Madarasa shule ya Msingi Mnyahi

 

Mwonekano wa ndani wa baadhi ya madarasa ya shule ya msingi Mnyahi iliyopo halmashauri ya mji Nanyamba mkoani Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa Mnyahi, Mtwara, wailalamikia Shule ya Msingi Mnyahi kuwa na majengo chakavu, wanafunzi kunyeshewa darasani,Wadai imepuuzwa licha ya ufaulu mzuri, viongozi waahidi hatua za ukarabati

Na Musa Mtepa

Wananchi wa Kijiji cha Mnyahi, kata ya Milangominne Halmashauri ya Mji Nanyamba mkoani Mtwara, wameiomba serikali kuangalia kwa jicho la tatu hali ya Shule ya Msingi Mnyahi kufuatia uchakavu wa majengo ya shule hiyo.Hali hiyo imeelezwa kusababisha wanafunzi kunyeshewa na mvua wakiwa darasani.

Wakizungumza na Jamii FM Radio Machi 28, 2026, wananchi hao wamesema licha ya shule hiyo kufanya vizuri kwa zaidi ya miaka kumi mfululizo katika mitihani ya Darasa la Saba, bado haijapatiwa ukarabati wala ujenzi wa majengo mapya.

Aidha, wameeleza kuwa shule hiyo imejengwa mwaka 1973, na mara ya mwisho kupata majengo mapya ilikuwa wakati wa utawala wa hayati Rais Benjamin Mkapa.

Sauti ya 1 Wananchi wa Mnyahi

Mkazi wa kijiji hicho, Abdulaaziz Bushiri Mjupa, amesema kutokana na serikali kutoipa kipaumbele shule hiyo katika ukarabati na ujenzi wa majengo, wananchi wamelazimika kuchangishana ili kupunguza baadhi ya changamoto, ikiwemo ujenzi wa matundu ya vyoo hali ambayo ni tofauti na ilivyo katika shule za vijiji jirani.

Sauti ya Abdulaaziz Bushiri mkazi wa Kijiji cha Mnyahi

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji hicho, Hamisi Salumu Mpangu, amekiri kuwepo kwa majengo yanayohitaji ukarabati mkubwa kutokana na uchakavu uliopitiliza.

Amesema tayari amewasilisha taarifa za hali hiyo katika vikao vya maendeleo ya kata zaidi ya mara tatu bila mafanikio yoyote.

Aidha, ametoa wito kwa viongozi wa halmashauri kufika kijijini hapo kujionea hali halisi na kuchukua hatua za haraka.

Sauti ya Hamisi Mpangu mwenyekiti wa Kijiji Mnyahi

Naye Diwani wa Kata ya Milangominne, Mhe. Sharifu Kapela, amesema kata hiyo ina shule mbili zenye changamoto ya majengo chakavu zinazohitaji ukarabati na ujenzi wa madarasa mapya.

Amezitaja shule hizo kuwa ni Milangominne na Mnyahi, akibainisha kuwa tayari ameshawasilisha suala hilo halmashauri na ameahidiwa kuwa litafanyiwa kazi kuanzia mwezi Agosti.

Pia ametoa wito kwa wadau wa maendeleo kujitokeza kusaidia kuboresha miundombinu ya shule hizo.

Sauti ya Mhe. Sharifu Kapela Diwani wa kata ya Milangominne

Akizungumzia suala hilo kwa njia ya simu, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Nanyamba, Hassani Ali Mauji, amekiri kuwepo kwa shule chakavu katika halmashauri hiyo.

Amesema shule hiyo imeingizwa katika mpango wa BOOST unaotarajiwa kuanza mwishoni mwa mwaka wa fedha wa serikali.

Sauti ya Hassani Ali Mauji mwenyekiti wa halmashauri ya Mji Nanyamba

Share:

Daraja lakatika, Namuhi, Mnyija wakosa mawasiliano

 

Mwonekano wa Daraja baada ya maji yanayotokea Bwawa la kitere kupitia mto Mambi kulivunja na wananchi kuunganisha kwa kutumia miti (Picha na Salamu Nayaula)

Na Musa Mtepa

Wananchi wa vijiji vya Namuhi na Mnyija wamejikuta katika wakati mgumu wa mawasiliano kufuatia kukatika kwa daraja linalounganisha vijiji hivyo, baada ya kufurika kwa maji yanayotoka Bwawa la Kitere kupitia Mto Mambi unaotenganisha maeneo hayo.

Wakizungumza na Jamii FM Radio Machi 28, 2026, wananchi hao wamesema kuwa uharibifu huo umetokana na maji mengi kufurika kutoka Bwawa la Kitere, hali ambayo imesababisha kusimama kwa baadhi ya shughuli za kiuchumi na kijamii, ikiwemo kilimo, usafirishaji pamoja na elimu.

Aidha, wameeleza kuwa kutokana na ulazima wa kuvuka katika eneo hilo, wamelazimika kuweka miti juu ya mto huo ili iwe njia ya kupita, jambo linalohatarisha usalama wao.

Sauti ya 1 Wananchi wa Mnyija

Hata hivyo, wananchi hao wameiomba serikali kufika katika eneo hilo kujionea hali halisi na kutatua changamoto hiyo ili kuepusha madhara zaidi yanayoweza kujitokeza.

Sauti ya 2 Wananchi wa Mnyija

Akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti wa Kijiji cha Namuhi, Mwenyekiti wa kitongoji katika eneo lilipo daraja lililokatika, Bi. Suluhisho Nammanga, amesema athari zinazotokana na hali hiyo ni pamoja na wanafunzi wa Shule ya Msingi Namuhi na Shule ya Sekondari Libobe kushindwa kuhudhuria masomo. Pia, baadhi ya wakulima wameshindwa kufika mashambani kwa kuwa mashamba yao yapo upande wa pili wa mto.

Sauti ya Bi Suluhisho Nammanga kaimu mwenyekiti

Aidha, Bi. Suluhisho ametoa wito kwa serikali kutembelea eneo hilo na kuona umuhimu wa kujenga daraja hilo kwa haraka ili huduma muhimu kwa wananchi ziweze kuendelea kama kawaida.

Pia ameishauri serikali kwamba daraja litakapojengwa liwe refu zaidi kuliko lilivyokuwa awali, na kusisitiza umuhimu wa kuhakikisha kuwa kazi ya mkandarasi inakidhi matakwa ya mkataba husika wakati wa ukaguzi na makabidhiano.

Sauti ya Bi Suluhisho Nammanga kaimu mwenyekiti
Share:

Panda shuka za Mariam kuitumikia Chuno

 

Mariam Chibwalo akizungumza na muandaaji wa makala haya, Picha na Mwanaidi Kopakopa

Je, viongozi huzaliwa au hutengenezwa na mazingira? Makala hii inachunguza mjadala huo kupitia Mariam Chibwalo, mwanamke aliyethubutu kusimama pekee yake dhidi ya wanaume tisa katika kinyang’anyiro cha udiwani. Akiwa amesukumwa na changamoto na hamasa ya kuwa sauti ya wananchi wa Chuno, Mariam anaonesha kuwa uongozi si ndoto tu bali ni uamuzi wa kusimama na kuwatumikia wengine.

Na Mwanahamisi Chikambu na Mwanaidi Kopakopa.

Nadharia za uongozi duniani zimegawanyika katika makundi mawili makuu. Kuna wanaoamini kuwa viongozi huzaliwa na wengine wanaosisitiza kuwa viongozi hutengenezwa na mazingira au matukio wanayokutana nayo maishani.

Wanaodai viongozi huzaliwa huamini kuwa kipaji cha kuongoza kimo ndani ya damu ya mtu tangu kuzaliwa. Kwa upande mwingine, wanaoamini kuwa mazingira humjenga kiongozi wanasema kuwa changamoto, kero na dhuluma ndizo humsukuma mtu kusimama kidete na kusema ”Sasa basi, mimi nitakuwa sauti ya wenzangu”.

Safari ya uongozi wa Mariam Chibwalo haikuwa nyepesi. Katika kinyang’anyiro cha udiwani, alijitosa akiwa mwanamke pekee akishindana na wanaume tisa. Wengi waliutafsiri ujasiri wake kama ndoto isiyowezekana, lakini kwake yeye, haikuwa tu siasa bali ilikuwa ni wito wa dhati wa kuwatumikia wananchi wa Chuno.

Karibu usikilize makala hii ya kusisimua… Bonyeza hapa.

Share:

TMA yasisitiza wakulima kutumia vizuri mvua zinazonyesha

 

Kaimu meneja TMA kanda ya kusini Elewa Msomba akiwa katika mahojiano kwenye kipindi cha Dira ya Asubuhi kinachorushwa na Jamii FM Radio Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wamehimizwa kutumia vizuri mvua zinazonyesha kwa shughuli za maendeleo huku wakitakiwa kuchukua tahadhari na kuzingatia ushauri wa wataalam wa hali ya hewa na kilimo ili kupata tija

Na Musa Mtepa

Wananchi wameshauriwa kutumia vizuri mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo yao kwa ajili ya shughuli za kimaendeleo, zikiwemo kilimo, uvuvi na ufugaji, ili kuwawezesha kupata tija.

Hayo yamesemwa Machi 23, 2026 na Kaimu Meneja wa TMA Kanda ya Kusini, Bw. Elewa Msomba, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Dira ya Asubuhi kinachorushwa na Jamii FM Radio. Amesema kuwa kwa kuwa msimu wa mvua unaelekea mwishoni katika ukanda wa kusini, wananchi hawana budi kuzitumia ipasavyo ili kupata manufaa katika shughuli zao.

Sauti ya 1 Elewa Msomba Kaimu Meneja TMA Kanda ya Kusini

Aidha, Bw. Elewa Msomba amesema kuwa pamoja na msimu wa mvua kuelekea ukingoni katika ukanda wa kusini, hasa kwa wanaoishi maeneo ya bondeni na yenye unyevunyevu, wanapaswa kuchukua tahadhari kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika kipindi hiki cha mwezi wa tatu ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza.

Sauti ya 2 Elewa Msomba Kaimu Meneja TMA Kanda ya Kusini

Kwa upande wake, Afisa Mfawidhi kutoka Kituo cha Hali ya Hewa kilichopo katika Kituo cha Utafiti wa Kilimo TARI–Naliendele, Renatus Kapenda, amewataka wakulima kulima mazao kwa kuzingatia utabiri wa hali ya hewa unaotolewa na TMA pamoja na ushauri wa wataalam wa kilimo waliopo katika maeneo yao, ili waweze kulima mazao yanayoendana na msimu husika.

Sauti ya 1 Renatus Kapenda Afisa TMA TARI–Naliendele

Sambamba na hilo, Renatus Kapenda amewataka wakulima kutambua kuwa mvua zinazoendelea kunyesha zinatarajiwa kuisha katika wiki ya nne ya mwezi Aprili na mwanzoni mwa mwezi Mei. Hivyo, ni muhimu kwa wakulima kuzingatia ushauri na kushirikiana na wataalamu wa kilimo ili kuelekezwa mbegu zinazofaa kulingana na kiasi cha mvua kilichobaki.

Sauti ya 2 Renatus Kapenda Afisa TMA TARI–Naliendele
Afisa mfawidhi kutoka kituo cha hali ya hewa katika kituo cha utafiti wa kilimo Tanzania TARI-Naliendele Renatus Kapenda akiwa katika studio za jamii fm radio (Picha na Musa Mtepa)

Kwa mujibu wa TMA, msimu wa mvua kwa mikoa ya kusini ulianza mwezi Disemba 2025 na unatarajiwa kumalizika katika wiki ya nne ya mwezi Aprili hadi wiki ya kwanza ya mwezi Mei, huku mvua hizo zikiwa chini ya wastani kulingana na rekodi za mvua katika mikoa hiyo.

Sauti ya 3 Elewa Msomba Kaimu Meneja TMA Kanda ya Kusini

Kusikiliza kipindi Bonyeza hapa

Share:

Sikiliza jamii FM Radio

🎧 Jamii FM Live

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

Blog Archive

WAENDESHA WEBSITE

Contact Form



1 ] )[0]; $title = $recent_post['post_title']; $excerpt = wp_trim_words( $recent_post['post_content'], 20 ); $image = get_the_post_thumbnail_url( $recent_post['ID'], 'full' ); ?>