• VIPINDI VYA ELIMU HASA KILIMO

    Tuna vipindi mbalimbali vinavyohamasisha jamii katika kilimo cha Korosho, ufuta na Mhogo. tunaendelea na jamii inafurahia uwepo wa vipindi kwa sababu wanakutana na wataalamu moja kwa moja

  • SAUTI ZA WANAJAMII HUSIKIKA

    Sauti ni muhimu hasa unapohudumia jamii ya vijijini, wasikilizaji hupenda kusikia sauti zao kwakua watu wao wanawafahamu, hivyo huwa kivutio kwako na ni rahisi jamii kuamini kuwa mpo pamoja nao

  • MICHEZO MBALIMBALI

    Afya ni sehemu ya vipindi vyetu kwenye radio, hii husaidia kuwapa fursa watu wanaopenda michezo kuwa pamoja na kubadirishana mawazo, michezo hujenga urafiki na undugu baina mwa jamii

  • WATOTO KATIKA RADIO

    Hupenda kushiriki na hujiona sehemu ya radio kwa kuwa huishi katika jamii, kipindi cha watoto kimekuwa kikifuatiliwa na watu wazima kwasababu kuu moja tu, watoto waishio vijijini huwa hawapewi kipaumbele kama tulivyofanya Jamii fm

  • SIKIKA KATIKA RADIO

    Kipengere hiki hutoa fursa kwa wanajamii wanaotuzunguka kuongea moja kwa moja na kueleza hoja zao ambazo baadae hufuatiliwa kwa undani

Vijana kata ya Chuno wahamasishwa kujipanga kiuchumi

 

Baadhi ya vijana wa kata ya Chuno Manispaa ya Mtwara Mikindani wakiwa katika Kongamano lililofanyika Jana January 25,2026 katika ofisi za kata ya hiyo(Picha na Henry Abdala)

Vijana wa Kata ya Chuno, Mtwara Mjini, wametakiwa kuungana katika vikundi ili kunufaika na tenda na mikopo ya serikali kwa maendeleo yao ya kiuchumi

Na Musa Mtepa

Vijana wametakiwa kuungana na kuunda vikundi vitakavyowawezesha kupata tenda na mikopo kutoka serikalini, hatua itakayosaidia kuinua uchumi wao binafsi na jamii kwa ujumla.

Wito huo umetolewa tarehe 25 Januari, 2026 na Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Mtwara MjiniNdugu Nassoro Mohemedi, wakati wa Kongamano la Vijana lililofanyika katika Kata ya Chuno.

Akizungumza katika kongamano hilo, Ndugu Mohemedi amesema kuwa vijana wana uwezo wa kujijenga kiuchumi ndani ya kipindi cha mwaka mmoja iwapo watajipanga vizuri na kutumia fursa za mikopo inayotolewa na halmashauri, sambamba na shughuli zao za kila siku.

Sauti ya Nassoro Mohamedi Mwenyekiti UVCCM Mtwara Mjini

Kwa upande wao, baadhi ya vijana waliohudhuria kongamano hilo wamesema wamejifunza mambo mbalimbali, ikiwemo kutambua fursa zilizopo katika maeneo yao. Aidha, wamewapongeza viongozi wa kata hiyo kwa kuwaandalia kongamano hilo lenye manufaa makubwa kwa maendeleo yao.

Sauti ya baadhi ya vijana wa kata ya Chuno

Naye mratibu wa kongamano hiloIddi wa Mangongo, kwa kushirikiana na Diwani wa Kata ya Chuno, amesema kuwa lengo kuu la kufanyika kwa kongamano hilo ni kutokana na kutambua kuwa vijana ni kundi kubwa na muhimu katika jamii, hivyo wanapaswa kuelimishwa na kupewa taarifa kuhusu fursa mbalimbali zinazopatikana katika maeneo yao.

Sauti ya Iddi wa Mangongo mratibu wa Kongamano
Share:

Wazazi wahimizwa kulea watoto kimaadili kuzuia mimba kwa wanafunzi

 

Baadhi ya wazazi wa kijiji cha Nanguruwe wakishiriki kipindi cha wazi juu ya ni kifanyike ili kutekeleza mimba kwa wanafunzi (Picha na Henry Abdala)

Wazazi wa kijiji cha Nanguruwe wameaswa kuwalea watoto wao katika maadili mema ili kukabiliana na mimba kwa wanafunzi. Wito huo umetolewa na viongozi wa elimu, polisi na walimu kupitia kipindi cha Wazi cha Jamii FM Redio.

Na Musa Mtepa

Wazazi wameshauriwa kuwalea watoto wao katika maadili mema ili kukabiliana na changamoto zinazowakabili wanafunzi, ikiwemo mimba za utotoni zinazosababisha baadhi yao kusitisha masomo wakiwa shuleni.

Ushauri huo umetolewa na Afisa Elimu Kata ya Nanguruwe, Omari Makiluli, aliposhiriki kipindi cha Wazi kinachorushwa na Jamii FM Redio tarehe Januari 17, 2026. Kipindi hicho kilifanyika katika eneo la stendi ya magari kijijini Nanguruwe, Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara mkoani Mtwara.

Akichangia mada iliyokuwa ikijadiliwa ya “Nini kifanyike ili kutekeleza sera na mikakati ya serikali juu ya kutokomeza mimba kwa wanafunzi”Makiluli amesema kumekuwepo na ombwe kubwa la wazazi na walezi katika kuwafuatilia mienendo ya watoto wao. Ameeleza kuwa ni muhimu wazazi kuwa karibu na watoto wao na kuwakuza katika maadili mema ili kuwaepusha na vishawishi vinavyoweza kuathiri maisha yao ya kielimu.

Sauti ya 1: Omari Makiluli, Afisa Elimu Kata ya Nanguruwe

Aidha, Afisa Elimu huyo amewasisitiza wazazi kuwahimiza watoto wao, hususan wa kike, kuendelea na masomo kwa kuhakikisha wanakwenda shule na kupata elimu itakayowawezesha kukabiliana na changamoto mbalimbali za kimaisha zinazojitokeza katika jamii.

Sauti ya 2: Omari Makiluli, Afisa Elimu Kata ya Nanguruwe

Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Nanguruwe, Mwalimu Keneth Kawinda, amesema kuwa ili kukabiliana na tatizo la mimba kwa wanafunzi, wazazi wanapaswa kuamini kuwa hosteli ni maeneo salama kwa watoto wao. Aidha amewataka wazazi kutoacha watoto wao uhuru wa kujiamulia kufanya mambo yasiyofaa bila usimamizi.

Sauti ya Mwalimu Keneth Kawinda, Kaimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Nanguruwe

Naye Afisa wa Jeshi la Polisi Kata ya Nanguruwe, WPO Titus Julius Godfrey, amesema utekelezaji wa sera na mikakati ya serikali juu ya kuondoa mimba kwa wanafunzi unahitaji ushirikiano wa karibu kati ya wazazi, walimu na wanafunzi wenyewe ili kuzungumza lugha moja na kumsaidia mtoto kufikia malengo yake ya kielimu.

Sauti ya WPO Titus Julius Godfrey, Afisa wa Jeshi la Polisi Kata ya Nanguruwe

Kwa upande wao, baadhi ya wazazi na wananchi waliohudhuria kipindi hicho wamekiri kutokuwa karibu vya kutosha na watoto wao, huku wengine wakiahidi kuanza upya kwa kuzungumza na watoto wao kuhusu umuhimu wa elimu na njia za kujiepusha na mimba wakiwa shuleni.

Sauti ya wazazi na wananchi wa Kijiji cha Nanguruwe

Kipindi cha Wazi kinachoratibiwa na Jamii FM Redio kilianza rasmi Oktoba 9, 2025 katika Kata ya Naliendele, Manispaa ya Mtwara Mikindani, kikiwa na mada isemayo “Nini kifanyike ili jamii ishiriki kikamilifu kupunguza tatizo la mimba kwa wanafunzi shuleni”, Januari 17, 2026 kimefanyika katika Kijiji cha Nanguruwe, Halmashauri ya wilaya ya Mtwara kilichokuwa na mada isemayo “Nini kifanyike ili kutekeleza sera na mikakati ya serikali kuzuia mimba kwa wanafunzi shuleni”, huku kipindi kijacho kinachotarajiwa kufanyika Januari 24, 2026 katika Kijiji cha Majengo, Kata ya Ziwani, kikijadili mada ya “Nini kifanyike ili shughuli za kiuchumi zisiwe chanzo cha wanafunzi kupata mimba na kuacha shule”.

Lengo kuu la vipindi hivi ni kutoa elimu kwa jamii, kuhimiza uwajibikaji kwa kila mmoja na kumwezesha mwanafunzi, hususan mtoto wa kike, kutimiza malengo yake kupitia elimu.

Share:

Wananchi wa Nanguruwe waomba msaada ujenzi wa Soko

 

Tofali zikiandaliwa kwa ajili ya ujezni wa Jengo la utawala la soko la kijiji cha Nanguruwe (Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa kijiji cha Nanguruwe wameiomba Serikali na wadau wa maendeleo kusaidia ujenzi wa soko la kisasa la bidhaa na vyakula ili kuboresha huduma za kibiashara. Ujenzi huo unafanywa kwa nguvu za wananchi na unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 70, huku wafanyabiashara zaidi ya 100 wakinufaika

Na Musa Mtepa

Wananchi wa kijiji cha Nanguruwe wameiomba Serikali pamoja na wadau wa maendeleo kuchangia na kusaidia ujenzi wa soko la bidhaa na vyakula unaoendelea kujengwa katika kijiji hicho.

Wakizungumza na Jamii FM Redio Januari 17, 2026, wananchi hao wamesema kuwa kutokana na ukuaji wa kasi wa kijiji chao, viongozi wa kijiji wameamua kuanzisha ujenzi wa soko la kisasa ili kuwaondolea adha wakazi wa kijiji hicho kutembea umbali mrefu kufuata huduma za kibiashara eneo la Barabarani.

Sauti ya wananchi wa kijiji cha Nanguruwe
Eneo linalotarajiwa kujengwa kwa soko la kijiji cha Nanguruwe (Picha na Musa Mtepa)

Akizungumza kuhusu ujenzi wa soko hilo, Mwenyekiti wa Kijiji cha Nanguruwe, Bw. Saidi Mandova, amesema kuwa sababu kubwa ya uamuzi huo ni matumizi ya soko moja kwa vijiji vitatu kwa muda mrefu, hali iliyokuwa ikikisababishia kijiji kukosa mapato yatokanayo na shughuli za kibiashara.

Bw. Mandova ameongeza kuwa ujenzi wa soko hilo unatekelezwa kwa nguvu za wananchi wenyewe, huku akiomba wadau wa maendeleo kujitokeza kusaidia ili kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati uliopangwa.

Sauti ya Mwenyekiti wa kijiji cha Nanguruwe

Kwa upande wake, Kaimu Mtendaji wa Kijiji cha Nanguruwe, Bw. Saidi Hamisi, ameelezea hatua za awali za utekelezaji wa mradi huo na kufafanua kuwa ujenzi unaendelea vizuri licha ya changamoto chache za upungufu wa rasilimali.

Ameongeza kuwa hadi kukamilika, ujenzi wa soko hilo unatarajiwa kugharimu shilingi milioni 70, huku zaidi ya wafanyabiashara 100 wakitarajiwa kunufaika na huduma za soko hilo.

Sauti ya Afisa Kaimu Mtendaji wa kijiji cha Nanguruwe
Eneo lililopangwa kwa ajili ya kujenga vibanda vya Wafanyabiashara katika soko la kijiji cha Nanguruwe(Picha na Musa Mtepa)
Share:

Serikali yataka kasi ujenzi barabara ya Mnivata-Masasi

 

Mkuu wa mkoa wa Mtwara Kanali Patrick Sawala akizungumza na wajumbe kwenye kikao cha Bodi ya Barabara kilichofanyika Januari 8, 2026 katika ukumbi wa BoT Kanda ya Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara ameitaka TANROADS kuongeza usimamizi kwa mkandarasi wa barabara ya Mnivata–Masasi baada ya mradi kusuasua. TANROADS imesema chanzo ni mkandarasi na hatua tayari zimechukuliwa kuharakisha ujenzi

Na Musa Mtepa

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrick Sawala, ameitaka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) Mkoa wa Mtwara kuendelea kumsimamia kikamilifu mkandarasi anayetekeleza mradi wa ujenzi wa barabara ya uchumi ya Mnivata–Tandahimba–Newala–Masasi yenye urefu wa kilomita 160 kwa kiwango cha lami, ili kuhakikisha unakamilika kwa wakati na kwa kuzingatia ubora unaotakiwa.

Kanali Sawala ametoa maelekezo hayo Januari 8, 2026, wakati wa kikao cha Bodi ya Barabara Mkoa wa Mtwara kwa mwaka wa fedha 2024/2025 na 2025/2026, kilichofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT) Kanda ya Mtwara, Manispaa ya Mtwara Mikindani.

Amesema utekelezaji wa mradi huo haujaenda kwa kasi ya kuridhisha, hali iliyomlazimu kuielekeza TANROADS kuongeza usimamizi kwa mkandarasi ili kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa ufanisi na kwa muda uliopangwa.

Sauti ya Kanali Patrick Sawala, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara

Kwa upande wao, Mbunge wa Jimbo la Nanyamba, Abdaa Dadi Chikota, pamoja na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Newala, Yusuf Kateule, wamehoji changamoto halisi inayomkabili mkandarasi huyo, wakitaka kufahamu iwapo kuchelewa kwa mradi kunasababishwa na ukosefu wa fedha au uzembe wa mkandarasi mwenyewe.

Sauti ya Mwenyekiti wa Halmashauri ya Newala na Mbunge Chikota

Akizungumzia kusuasua kwa mradi huo, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mtwara, Emil Zengo, amesema tayari wamemwondoa msimamizi mkuu wa mkandarasi na kumleta msimamizi mwingine, ikiwa ni sehemu ya hatua za kuharakisha utekelezaji wa ujenzi wa barabara hiyo.

Aidha, amesema kuwa kuhusu ujenzi wa barabara za mchepuko, amemuelekeza mhandisi mshauri kumkata mkandarasi malipo yanayohusiana na kazi ambazo hazijatekelezwa kwa viwango vinavyotakiwa.

Sauti ya 1 Emil Zengo, Meneja TANROADS Mkoa wa Mtwara
Meneja TANROADS Mkoa wa Mtwara Emil Zengo akiwasilisha hali ya Barabara na utekelezaji wa miradi Mbalimbali inayotekelezwa katika mkoa wa Mtwara(Picha na Musa)

Akijibu maswali kutoka kwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Newala na Mbunge wa Nanyamba kuhusu iwapo chanzo cha kusuasua kwa mradi huo ni fedha au mkandarasi, Meneja wa TANROADS amesema chanzo kikuu ni mkandarasi, huku akisisitiza kuwa hatua stahiki tayari zimechukuliwa kurekebisha hali hiyo.

Sauti ya 2 Emil Zengo, Meneja TANROADS Mkoa wa Mtwara

Kwa upande wake, Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mtwara, Ibrahim Mjanakheri Ibrahim, akizungumza kwa niaba ya Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoa, amesema CCM inaunga mkono azimio la kuitaka TANROADS kuharakisha kwa kasi zaidi ujenzi wa barabara hiyo ya uchumi kutokana na umuhimu wake katika kuchochea maendeleo ya wananchi wa Mkoa wa Mtwara.

Katibu wa CCM Mkoa wa Mtwara Ibrahim Mjanakheri Ibrahim akizungumza na wajumbe wa kikao cha Bodi ya barabara kilichofanyika Januari 8,2026 katika ukumbi wa BOT kanda ya Mtwara(Picha na Musa Mtepa)
Share:

Wananchi Makome B: Maji yalitoka dakika tano tu

 

Tanki la maji liliojengwa katika kijiji cha Makome B ambao ni mradi unaohusisha vijiji viwili vya Makome A na B ambao ujenzi wake umefikia asilimia 65(Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa Makome B wameiomba Serikali kupitia RUWASA kukamilisha mradi wa maji uliosimama ili kumaliza uhaba wa maji safi unaosababisha magonjwa na changamoto za kijamii.

Na Musa Mtepa

Wananchi wa kijiji cha Makome B kilichopo kata ya Mbawala,Halmashauri ya Mtwara vijijini, Mkoani Mtwara wameiomba Serikali kupitia Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kukamilisha mradi wa maji unaojengwa katika kijiji hicho ili kuondokana na adha ya uhaba wa maji safi na salama inayowakabili.

Wakizungumza na waandishi wa habari January 6 ,2026 wananchi hao wamesema kuwa kutokana na kukosekana kwa maji safi na salama, wamekuwa wakikumbana na changamoto mbalimbali za kiafya na kijamii, hali inayotokana na matumizi ya vyanzo vya maji vya asili ambavyo si salama kwa matumizi ya binadamu.

Wakazi wa kijiji hicho, Mwanahamisi Mitole na Sinani Kibwana, wamesema tatizo la maji limesababisha kuongezeka kwa magonjwa ya tumbo, hatari ya kushambuliwa na wanyama wakali pamoja na migogoro ya kifamilia, hali inayohatarisha ndoa zao. Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wameomba wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) kukamilisha mradi wa maji uliosimama katika kijiji hicho.

Sauti ya Mwanahamisi Mitole na Sinana Kibwana, wakazi wa Makome B
Wananchi wa kijiji cha Makome B wakiteka Maji katika kisima cha asili kilichopo kijijini hapo(Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B, Ndugu Salumu Liwingu, amekiri kuwa hali ya upatikanaji wa maji safi na salama katika kijiji hicho ni mbaya, kwani wananchi wanategemea maji yanayotiririka kutoka maeneo mbalimbali ambayo si salama, hali inayochangia wananchi kupata magonjwa ya tumbo mara kwa mara.

Sauti ya Salumu Liwingu, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B
Salumu Liwingu, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B(Picha na Musa Mtepa)

Akizungumzia mradi wa maji unaojengwa kijijini hapo, Mwenyekiti huyo amesema mradi huo umeingia mwaka wa tatu tangu kuanza kwake. Ameeleza kuwa mradi huo ulizinduliwa rasmi mwaka 2024 wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru, lakini maji yalitoka kwa takribani dakika tano pekee na tangu hapo hakuna maji yaliyowahi kutoka tena.

Sauti ya Salumu Liwingu, Mwenyekiti wa kijiji cha Makome B

Kwa upande wake, Kaimu Meneja wa wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Wilaya ya Mtwara, Abdulaziz Hemedi, amesema mradi wa maji wa Makome umefikia asilimia 65 ya utekelezaji, huku asilimia 41 ya fedha za mradi zikiwa tayari zimeshalipwa kwa mkandarasi. Amesema changamoto mbalimbali zimejitokeza na kusababisha mradi huo kushindwa kutoa huduma ya maji kwa wananchi wa Makome A na B, hali iliyopelekea RUWASA kufikiria kuvunja mkataba na mkandarasi husika.

Sauti ya Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Mtwara
Mwonekano wa kisima cha asili cha maji kinachotumiwa na wananchi wa Makome B kunywa,kuoshea na kuogea(Picha na Musa Mtepa)

Aidha, amesema mkataba wa ujenzi na ukamilishaji wa mradi huo ulitarajiwa kukamilika mwezi Novemba 2025, na kufikia wakati wanapofikiria kuvunja mkataba, utekelezaji ulikuwa umefikia asilimia 65.

Sauti ya Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Mtwara
Mwonekano wa baadhi ya Bomba zilizo telekezwa porini baada ya mkandarasi wa kutokamilisha ujenzi wa mradio huo(Picha na Musa Mtepa)

Hata hivyo, Kaimu Meneja huyo amesema pamoja na mchakato wa kuvunja mkataba na kumpata mkandarasi mpya wa kukamilisha mradi huo, wananchi wa vijiji vya Makome A na B wanatarajiwa kupata huduma ya maji safi na salama ndani ya kipindi cha miezi mitatu ijayo.

Sauti ya Kaimu Meneja wa RUWASA Wilaya ya Mtwara

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Wizara ya Maji na ofisi mbalimbali za Serikali, hadi kufikia mwezi Julai 2025 upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika maeneo ya vijijini umefikia asilimia 83 na Sera ya Taifa ya Maji ikisisitiza upatikanaji endelevu wa maji safi na salama kwa kuhusisha jamii, sekta binafsi pamoja na kulinda rasilimali za maji ili kuhakikisha huduma hiyo inawafikia wananchi wote wa vijijini.

Wananchi wa kijiji cha Makome B wakiwa njiani kuelekea Nyumbani wakitokea Kisimani kuteka maji(Picha na Musa Mtepa)
Share:

Wahitimu Mtwara Ufundi wachangia ujenzi wa msikiti Mtwara

 

Eneo linalotarajiwa kujenga Msikiti katika mtaa wa Shule ya msingi Majengo kata ya Tandandika Manispaa ya Mtwara Mikindani (Picha na Musa Mtepa)

Wanafunzi waliowahi kusoma Shule ya Sekondari Mtwara Ufundi wamechangia shilingi 525,000/= kwa ajili ya ujenzi wa Msikiti wa mtaa wa Shule ya Msingi Majengo, Manispaa ya Mtwara

Na Musa Mtepa

Wanafunzi waliowahi kusoma Shule ya Sekondari Mtwara Ufundi iliyopo Manispaa ya Mtwara ya Mikindani, wamechangia jumla ya shilingi laki tano na elfu ishirini na tano (525,000/=) kwa ajili ya ujenzi wa msikiti wa mtaa wa shule ya msingi Majengo.

Akizungumza leo Januari 5, 2026 mara baada ya kukabidhi mchango huo katika eneo linalotarajiwa  ujenzi wa Msikiti huo, mwanajumuia wa wanafunzi hao, Hamdani Swalehe Amlima, amesema kuwa wao kama wadau waliamua kuwashirikisha wenzao waliowahi kusoma Shule ya Sekondari Mtwara Ufundi ili kuona namna wanavyoweza kusaidia ujenzi huo, hatua iliyowezesha kupatikana kwa mchango huo.

Sauti ya Hamdani Swalehe Amlima – Mwanajumuia
Mwanajumuia ya wanafunzi waliowahi kusoma shule ya Sekondari Mtwara Ufundi akikabidhi fedha shilingi 525,000/= kwa mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa Msikiti(Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Msikiti huo, Mzee Musa Napinda, ameishukuru jumuia hiyo kwa mchango wao akisema kuwa fedha hizo zitasaidia kwa kiasi kikubwa katika hatua za awali za ujenzi wa Msikiti huo.

Aidha, Mzee Napinda ametumia fursa hiyo kuwaomba wadau wa maendeleo pamoja na waumini mbalimbali kujitokeza kuchangia ujenzi wa Msikiti huo ili kuwasaidia waumini wa Kiislamu katika eneo hilo kupata sehemu ya karibu ya kufanyia ibada.

Sauti ya Mzee Musa Napinda – Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Msikiti

Nao baadhi ya viongozi na waumini wa mtaa wa Shule ya Msingi Majengo wameishukuru jumuia hiyo pamoja na Diwani wa kata hiyo kwa kuhamasisha na kufanikisha upatikanaji wa mchango huo, huku wakiomba taasisi, wadau na waumini wengine kujitokeza ili kufanikisha ujenzi wa Msikiti huo.

Sauti ya waumini na viongozi wa mtaa unaojengwa Msikiti
Mhe; Diwani wa kata ya Tandika Al-Hajji Haroun Selemani Haroun akiwa na baadhi ya viongozi wa kamati ya ujenzi wa Msikiti wa mtaa wa Shule ya Msingi Majengo(Picha na Musa Mtepa)

Naye Diwani wa Kata ya Tandika, ambako Msikiti huo unatarajiwa kujengwa, Al-Hajji Haroun Selemani Haroun maarufu kama Chai Jaba, amewashukuru wakazi wa mtaa wa Shule ya Msingi Majengo pamoja na wanajumuia wa Mtwara Ufundi kwa moyo wao wa kujitolea na kushiriki katika kutoa sadaka hiyo (Swadakati Jaria).

Sauti ya Al-Hajji Haroun Selemani Haroun – Diwani wa Kata ya Tandika
Share:

Sikiliza jamii FM Radio

🎧 Jamii FM Live

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

Blog Archive

WAENDESHA WEBSITE

Contact Form



1 ] )[0]; $title = $recent_post['post_title']; $excerpt = wp_trim_words( $recent_post['post_content'], 20 ); $image = get_the_post_thumbnail_url( $recent_post['ID'], 'full' ); ?>