• VIPINDI VYA ELIMU HASA KILIMO

    Tuna vipindi mbalimbali vinavyohamasisha jamii katika kilimo cha Korosho, ufuta na Mhogo. tunaendelea na jamii inafurahia uwepo wa vipindi kwa sababu wanakutana na wataalamu moja kwa moja

  • SAUTI ZA WANAJAMII HUSIKIKA

    Sauti ni muhimu hasa unapohudumia jamii ya vijijini, wasikilizaji hupenda kusikia sauti zao kwakua watu wao wanawafahamu, hivyo huwa kivutio kwako na ni rahisi jamii kuamini kuwa mpo pamoja nao

  • MICHEZO MBALIMBALI

    Afya ni sehemu ya vipindi vyetu kwenye radio, hii husaidia kuwapa fursa watu wanaopenda michezo kuwa pamoja na kubadirishana mawazo, michezo hujenga urafiki na undugu baina mwa jamii

  • WATOTO KATIKA RADIO

    Hupenda kushiriki na hujiona sehemu ya radio kwa kuwa huishi katika jamii, kipindi cha watoto kimekuwa kikifuatiliwa na watu wazima kwasababu kuu moja tu, watoto waishio vijijini huwa hawapewi kipaumbele kama tulivyofanya Jamii fm

  • SIKIKA KATIKA RADIO

    Kipengere hiki hutoa fursa kwa wanajamii wanaotuzunguka kuongea moja kwa moja na kueleza hoja zao ambazo baadae hufuatiliwa kwa undani

Jamii FM yatoa tuzo kwa wasikilizaji bora wa mwaka 2025

 

Mkurugenzi wa jamii fm radio Ndug Swallah Saidi Swallah akiwa katika picha ya pamoja na washindi wa tuzo,wasikilizaji wa vipindi na wafanyakazi wa kituo hicho(Picha na Mohamedi Masanga)

Jamii FM Redio imetangaza wasikilizaji na wachangiaji bora wa vipindi vyake kwa mwaka 2025. Washindi walichaguliwa na wasikilizaji kupitia SMS na kukabidhiwa tuzo katika hafla iliyofanyika katika studio za kituo hicho

Na Musa Mtepa

Jamii FM Redio imetangaza wasikilizaji na wachangiaji bora wa vipindi vyake kwa mwaka 2025, katika hafla iliyofanyika Jumatano Desemba 31, 2025, katika kituo cha kurushia matangazo cha Jamii FM Redio kilichopo Mtwara.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mkurugenzi wa Jamii FM Redio, Bw. Swallah Said Swallah, alimtangaza Ndg. Mambo Katani, mtoto wa Fatu Mohamedi Kumbuko kutoka kijiji cha Rondo Ntene, Halmashauri ya Mtama mkoani Lindi, kuwa msikilizaji na mchangiaji bora wa kiume. Aidha, Bi. Amina Mkanjima, binti wa Mkanjima maarufu kama Mama wa Yanga (Mama Bakari Kitemwe) kutoka Manispaa ya Mtwara Mikindani, alitangazwa kuwa msikilizaji na mchangiaji bora wa kike.

Sauti ya Swallah Said Swallah, Mkurugenzi wa Jamii FM Redio

Bw. Swallah amesema kuwa utaratibu wa kutambua na kuwazawadia wasikilizaji na wachangiaji bora ulianza rasmi mwaka 2024 na utaendelea kila mwaka, huku kituo kikiendelea kuboresha mifumo ya upatikanaji wa washindi pamoja na thamani ya zawadi zitakazotolewa kadri miaka inavyoendelea.

Sauti ya Swallah Said Swallah, Mkurugenzi wa Jamii FM Redio

Akizungumzia malengo ya kituo hicho, Bw. Swallah ameeleza kuwa kuanzishwa kwa Jamii FM chini ya MTUKWAO Community Media kunalenga kuibua, kuchakata na kurusha taarifa za kijamii ambazo mara nyingi hazipewi nafasi katika vyombo vingine vya habari na kubainisha kuwa lengo la MTUKWAO COMMUNITY MEDIA kuwa na kituo hicho cha redio na televisheni ya kijamii (Community Television – CTV).

Sauti ya Swallah Said Swallah, Mkurugenzi wa Jamii FM Redio

Uchaguzi wa washindi ulifanyika kwa kuwashirikisha wasikilizaji wenyewe kupitia ujumbe mfupi wa maandishi (SMS), ambapo walipiga kura kumchagua msikilizaji na mchangiaji bora wa kike na wa kiume.

Nao baadhi ya washiriki waliofanikiwa kufika hatua ya washiriki 15 bora wameipongeza Jamii FM Redio kwa kuandaa tuzo hizo, wakieleza kuwa hatua hiyo imeongeza hamasa ya ushiriki wa vipindi na kuwapongeza washindi waliopata tuzo kwa mwaka 2025.

Sauti ya washiriki wa tuzo za uchangiaji na usikilizaji bora

Kwa upande wao, Bi. Amina Mkanjima na Ndg. Mambo Katani, washindi wa tuzo za msikilizaji na mchangiaji bora kwa mwaka 2025, wameishukuru Jamii FM Redio pamoja na wasikilizaji wote kwa kuwaamini na kuwachagua. Pia wametoa wito kwa wasikilizaji wengine kuendelea kufuatilia na kuchangia vipindi vya redio hiyo kwa kuzingatia maadili, utaratibu na kuheshimu haki za wengine bila kumdhuru mtu yeyote.

Sauti ya washindi wa tuzo

Naye Meneja wa Jamii FM Redio, Bw. Amua Rushita, amewashukuru wasikilizaji wa Jamii FM Redio kwa kuendelea kuisikiliza redio hiyo kwa mwaka 2025, huku akiukaribisha mwaka 2026 kwa kauli mbiu isemayo “Mtaa kwa Mtaa.”

Jumla ya washiriki kumi na tano (15) walichaguliwa kufikia hatua ya mwisho ya mashindano, ambapo wawili kati yao waliibuka washindi.

Washindi wamekabidhiwa zawadi ya redio aina ya Subwoofer yenye thamani ya shilingi laki moja na elfu hamsini (Tshs 150,000/=) kila mmoja.

Share:

Ni lini MV Kilambo itarejea?

 

Watumiaji wa kivuko cha Mv Kilambo wakilazimika kuvuka kwa kutumia Boti ndogo kulekea nchi jirani ya Msumbiji(Picha na Musa Mtepa)

Wananchi wa Kilambo na maeneo ya mpakani na Msumbiji wanaiomba Serikali kurejesha kivuko cha MV Kilambo kilichosimama kufanya kazi, Serikali imesema matengenezo yanaendelea

Na Musa Mtepa

Wananchi na watumiaji wa kivuko cha Kilambo kinachounganisha Tanzania na nchi jirani ya Msumbiji wamehoji ni lini kitarejea na kuiomba Serikali kuchukua hatua za haraka kurejesha huduma ya feri ya MV Kilambo, ili kuondoa usumbufu na gharama kubwa wanazokumbana nazo kwa sasa.

Wakizungumza na waandishi wa habari, wakazi wa eneo hilo wamesema hali ya usafiri si ya kuridhisha, kwani wanalazimika kutumia viboti vidogo kuvuka mpaka wa maji, ambavyo si salama na vina gharama kubwa ikilinganishwa na huduma ya awali ya feri.

Ahamadi Hassani na Ahamadi Fuka, wakazi wa Kijiji cha Kilambo katika Halmashauri ya Mtwara Vijijini, wanasema kutokuwepo kwa feri hiyo kunawalazimu kutumia vyombo vya majini visivyo salama, hali inayohatarisha maisha yao na kuongeza gharama za usafiri.

Sauti: Ahamadi Hassani na Ahamadi Fuka – Wakazi wa Kijiji cha Kilambo

Kwa upande wake, Rajabu Athumani Salumu, dereva wa bodaboda kutoka kijiji hicho, amesema ukosefu wa chombo cha uhakika cha usafiri umesababisha mlundikano wa abiria na mizigo, huku baadhi ya wasafiri wakilazimika kulala eneo hilo kwa zaidi ya siku tatu wakisubiri usafiri.

Sauti: Rajabu Athumani Salumu – Bodaboda, Kijiji cha Kilambo
Baadhi ya bidhaa zinazovushwa kupitia kivuko cha Kilambo kuelekea Palma na vijiji jirani vya Msumbiji(Picha na Musa Mtepa0

Naye Fatuma Bakari, mkazi wa Kijiji cha Singa kilichopo nchini Msumbiji, amesema ucheleweshaji unaotokana na kutokuwepo kwa kivuko hicho ni changamoto kubwa kwa wakazi wa pande zote mbili za mpaka, hasa kwa shughuli za kibiashara na kijamii.

Sauti: Fatuma Bakari – Mkazi wa Kijiji cha Singa, Msumbiji

Akitoa ufafanuzi kwa njia ya simu, Meneja wa Vivuko Kanda ya Mashariki na Kusini, Abdulrahman Amir, amesema feri ya MV Kilambo ilipelekwa kufanyiwa matengenezo, lakini baada ya kukamilika ilirejeshwa Mtwara Mjini kutokana na changamoto za kiusalama na miundombinu katika eneo la Kilambo–Namoto kwa kipindi hicho.

Sauti: Abdulrahman Amir – Meneja wa Vivuko Kanda ya Mashariki na Kusini
Viroba vya unga vya wafanyabiashara wa Msumbiji wakisubiria Boti ili waweze kuvusha kuelekea nchini Msumbiji( Picha na Musa Mtepa)

Ameongeza kuwa kutokana na kivuko hicho kukaa muda mrefu bila kufanya kazi, kinahitaji kufanyiwa marekebisho makubwa pamoja na kuboreshwa kwa miundombinu ya kuegeshea feri katika eneo la Kilambo.

Aidha, amesema TEMESA inatarajia kuingia mkataba kwa ajili ya matengenezo hayo makubwa, huku matarajio ya kurejea kwa huduma ya kivuko cha MV Kilambo kwa wananchi yakiwa ni kuanzia mwishoni mwa mwezi Februari mwaka 2026.

Sauti: Abdulrahman Amir – Meneja wa Vivuko Kanda ya Mashariki na Kusini
Share:

Bei ya korosho yazua sintofahamu Nanyamba

 

Mwonekano wa korosho ikiwa kwenye mti kabla ya kudondoka (Picha na Musa Mtepa)

Wakulima wa korosho Nanyamba wamelalamikia tofauti kubwa ya bei ukilinganisha na Tandahimba, hali inayowalazimisha kuhamishia mazao yao Tandahimba

Na Musa Mtepa

Wakulima  wa zao la korosho katika Halmashauri ya Mji Nanyamba wamehoji tofauti ya bei ya korosho inayojitokeza sokoni kati ya halmashauri hiyo na Wilaya ya Tandahimba, hali inayowalazimu baadhi yao kupeleka mazao yao Tandahimba ili kupata bei ya juu zaidi.

Wakizungumza na waandishi wa habari, wakulima hao wamesema kuwa kwa takribani miaka kumi sasa bei ya korosho imekuwa hairidhishi, huku tofauti ya bei kati ya Nanyamba na Tandahimba ikiendelea kuwa kubwa.

Wamesema kuwa licha ya madai ya kuwepo kwa unyevu kwenye korosho zinazouzwa Nanyamba, korosho hizo hizo zikipelekwa Tandahimba hununuliwa kwa bei ya juu zaidi.

Sauti ya 1: Wakulima wa korosho Nanyamba

Wakizungumzia sababu za utofauti wa bei ndani ya mnada mmoja, wakulima hao wamesema kuwa mfumo wa ununuzi wa korosho kwa njia ya loti unaochangia tofauti ya bei kati ya Halmashauri ya Nanyamba na maeneo mengine ya Mtwara, Masasi pamoja na Nanyumbu.

Sauti ya 2: Wakulima wa korosho Nanyamba

Jamali Nalyogo, mkulima kutoka Mtimbwilimbwi, pamoja na Issa Kamkunje wa kijiji cha Njengwa wamesema hali hiyo imekuwa ikiwasababishia maumivu ya moyo, huku wakilaumu wawakilishi (Wabunge)  na viongozi wanaosimamia zao la korosho katika Halmashauri ya Nanyamba,Mtwara,Masasi na Nanyumbu kutowatendea haki.

Sauti ya 3: Jamali Nalyogo na Issa Kamkunje – wakulima

Kwa upande wake, Meneja wa Chama Kikuu cha Ushirika cha MAMCU, Biadia Mtipa, amesema kuwa wakulima wa Nanyamba wako karibu na ukanda wa bahari hali inayosababisha korosho zao kuwa na unyevu mkubwa, jambo linalopunguza ubora na hatimaye kushusha bei sokoni.

Sauti ya Biadia Mtipa – Meneja MAMCU
Share:

Zimamoto Mtwara yatoa elimu matumizi sahihi ya Gesi majumbani

 

Mrakibu msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji mkoa wa Mtwara Ambros Ndunguru akiwa katika studio za jamii fm redio akitoa elimu ya matumizi sahihi ya Gesi ya kupikia majumbani(Picha na Amua Rushita)

Wananchi wametakiwa kuzingatia matumizi sahihi ya gesi ya kupikia majumbani ili kuepuka madhara ikiwemo milipuko ya moto

Na Musa Mtepa

Wananchi wameshauriwa kuzingatia matumizi sahihi ya gesi ya kupikia majumbani ili kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza, ikiwemo milipuko ya moto inayosababishwa na matumizi yasiyo salama ya nishati hiyo.

Ushauri huo umetolewa leo Disemba 24, 2025 na Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mtwara, Ambros Ndunguru, alipokuwa akizungumza katika kipindi cha Dira ya Asubuhi kinachorushwa na Jamii FM Redio.

Ndunguru amesema kuwa, mteja anaponunua gesi dukani, anatakiwa kwanza kuhakikisha anapima uzito wa mtungi wa gesi husika, pamoja na kuzingatia namna sahihi ya kuusafirisha. Ameongeza kuwa baada ya kuufikisha nyumbani, ni vyema kusubiri angalau dakika 30 kabla ya kuanza kuutumia.

Sauti ya 1: Ambros Ndunguru, Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji

Aidha, Ndunguru amesema kuwa kutokana na kuimarika kwa kitengo cha huduma na mawasiliano, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limekuwa likipokea taarifa nyingi kutoka kwa wananchi kuhusu matukio mbalimbali yanayosababishwa na mitungi ya gesi.

Sauti ya 2: Ambros Ndunguru, Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji

Akizungumzia hatua zinazopaswa kuchukuliwa endapo gesi itavuja au kulipuka, Ndunguru amesema kuwa ni muhimu kuepuka kuwasha au kuzima swichi za umeme, pamoja na kuto-buruta kitu chochote chenye uwezo wa kuzalisha cheche, kwani kufanya hivyo kunaweza kusababisha mlipuko mkubwa zaidi.

Sauti ya 3: Ambros Ndunguru, Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji

Hata hivyo, ametoa wito kwa wananchi kuendelea kuzingatia matumizi sahihi ya gesi ya kupikia majumbani, sambamba na kuwasiliana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kupiga simu ya bure 114 kwa ajili ya kupata elimu zaidi au kutoa taarifa za matukio mbalimbali ya uokoaji.

Sauti ya 4: Ambros Ndunguru, Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji

Kusikiliza kipindi chote Bonyeza hapa

Share:

Watu wenye ulemavu na mazingira

Msafiri kipila akiwa na Fransis Chiwango katika mahojiano ya kipindi hiki. Picha na Mwandishi wetu

Ulemavu si jambo la hiari, na kwamba mtu yeyote anaweza kuwa mlemavu wakati wowote katika maisha yake.

Na Msafiri Kipila

Watu wenye ulemavu ni sehemu muhimu ya jamii na wana mchango mkubwa katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi. Licha ya uwezo na vipaji walivyonavyo, kundi hili limekuwa likikumbana na changamoto mbalimbali, nyingi zikiwa ni za kuepukika. Changamoto hizo ni pamoja na miundombinu isiyo rafiki, ukosefu wa mazingira jumuishi, pamoja na kukosekana kwa usawa wa fursa katika nyanja mbalimbali za maisha.

Kwa kutambua hali hiyo, wanachuo wa Chuo cha Utumishi wa Umma wametoa maoni yao kuhusu umuhimu wa kuboresha mazingira yanayowazunguka watu wenye ulemavu. Wanachuo hao wamejadili pia namna bora za kutatua changamoto wanazokumbana nazo watu wenye ulemavu, wakisisitiza kuwa ulemavu si jambo la hiari, na kwamba mtu yeyote anaweza kuwa mlemavu wakati wowote katika maisha yake.

Bonyeza hapa kusikiliza

Share:

TARURA Mtwara yaianza miradi ya TACTIC ya bilioni 27.4

 

Maandalizi ya ujenzi wa ofisi za TARURA na Maabara ya kupimia vifaa na miradi ya ujenzi wilaya ya Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

TARURA Wilaya ya Mtwara imeanza utekelezaji wa miradi ya TACTIC ikihusisha ujenzi wa ofisi, maabara ya kupima ubora wa miradi, barabara na mifereji ya maji, huku ikilenga kuboresha miundombinu na kutoa ajira kwa wananchi wa eneo hilo

Na Musa Mtepa

TARURA Wilaya ya Mtwara imeanza utekelezaji wa miradi ya Uboreshaji wa Miundombinu ya Miji ya Tanzania (TACTIC) inayofadhiliwa na Serikali Kuu kupitia mkopo wa Benki ya Dunia, kwa kuanza ujenzi wa jengo la ofisi ya usimamizi wa miradi pamoja na maabara ya kupima ubora wa vifaa vya ujenzi na miradi.

Akizungumza na waandishi wa habari Desemba 22, 2025 katika eneo la mradi, Meneja wa TARURA Wilaya ya Mtwara, Mhandisi Hatibu Nunu, amesema mradi huo unagharimu shilingi bilioni 27.4 na unatekelezwa na Mkandarasi Serengeti Limited. Amesema ujenzi huo umeanza rasmi Desemba 5, 2025 na utahusisha ujenzi wa ofisi tatu pamoja na chumba maalumu cha Maabara.

SAUTI: Mhandisi Hatibu Nunu – Meneja TARURA Wilaya ya Mtwara

Mhandisi Nunu ameongeza kuwa miradi ya TACTIC pia inahusisha ujenzi wa Barabara ya Pacha ya Mbae yenye urefu wa kilomita 2.4, Barabara ya stendi ya Chipuputa yenye urefu wa kilomita 2.4, Barabara ya kuzunguka soko la Chuno yenye urefu wa kilomita 3 pamoja na ujenzi wa mifereji ya maji ya mvua.

SAUTI: Mhandisi Hatibu Nunu – Meneja TARURA Wilaya ya Mtwara

Kwa upande wa ukarabati wa Barabara, amesema Wilaya ya Mtwara hutengewa shilingi bilioni 7 kwa mwaka kwa ajili ya halmashauri tatu, ambapo Manispaa ya Mtwara Mikindani hupata shilingi bilioni 3.8. Kwa mwaka huu, TARURA imesaini mikataba yenye thamani ya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ukarabati wa Barabara na usafishaji wa mifereji, kazi ambazo tayari zinaendelea.

SAUTI: Mhandisi Hatibu Nunu – Meneja TARURA Wilaya ya Mtwara

Naye Mhandisi Mshauri Mkazi wa miradi ya TACTIC katika Manispaa ya Mtwara Mikindani, Henry Moshi, amesema mkandarasi yupo katika hatua za maandalizi ya kazi (mobilization) na ameahidi kuwa vibarua wazawa watapewa kipaumbele katika ajira.

SAUTI: Mhandisi Henry Moshi – Mshauri wa Miradi ya TACTIC

Nao wananchi wakiwemo vijana na mama lishe wameeleza kufarijika na uwepo wa miradi hiyo wakisema italeta tija, kuongeza kipato na kuboresha mazingira ya biashara, huku wakiwahimiza vijana kutumia fursa zinazojitokeza.

SAUTI: Vijana na Mama Lishe
Share:

FPCT Mtwara yawapatia watoto zawadi za Krismasi

 

Baadhi ya watoto na vijana wanaonufaika na kituo cha maendeleo ya mtoto na vijana cha FPCT Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

Kituo cha Maendeleo ya Mtoto na Kijana FPCT Mtwara kimetoa zawadi za Krismasi kwa watoto wanaosoma kituoni hapo, ikiwa ni kuwapongeza na kumshukuru Mungu

Na Musa Mtepa

Kituo cha Maendeleo ya Mtoto na Kijana cha FPCT Mtwara kimetoa zawadi za Krismasi kwa watoto wanaosoma katika Kituo cha Huduma ya Mtoto, ikiwa ni sehemu ya kumshukuru Mungu na kuwapongeza watoto hao kwa juhudi zao katika masomo.

Akizungumza leo Disemba 20, 2025 wakati wa zoezi la utoaji wa zawadi hizo, Mchungaji Kiongozi Msaidizi wa Kanisa la FPCT Mtwara, Frank Mchihama, amesema pamoja na utoaji wa zawadi, kituo hicho kimezindua utaratibu mpya wa ufadhili wa ndani, utakaosaidia kukusanya fedha kwa ajili ya kuwafikia watoto wengine waliopo katika mazingira magumu ambao bado hawajapata fursa ya kuhudumiwa na kituo hicho.

Sauti ya 1: Frank Mchihama, Mchungaji Kiongozi Msaidizi FPCT Mtwara
Mchungaji Kiongozi Msaidizi wa Kanisa la FPCT Mtwara, Frank Mchihama akielezea juu ya uzinduzi wa ufadhili wa ndani (Picha na Musa Mtepa)

Kwa upande wake, Afisa mawasiliano na fedha wa Kituo hicho, Bi Dorcas Mlawa, amesema zawadi zilizotolewa zimegharimu jumla ya shilingi milioni sita. Ameeleza kuwa katika kipindi cha miaka 10 ya uendeshaji wa kituo, wamepata mafanikio makubwa ikiwemo kuwasaidia watoto kufikia viwango mbalimbali vya elimu kama vile kidato cha sita, vyuo vya kati pamoja na vyuo vikuu.

Sauti ya 1: Dorcas Jackson, Meneja wa Kituo
Afisa mawasiliano na fedha Bi Dorcas Mlawa akielezea juu ya mafanikio ya kituo (picha na Musa Mtepa)

Aidha, Bi Dorcas amesema kituo hicho hakibagui watoto, kwani kinapokea watoto kutoka jamii zote bila kujali imani, rangi au kabila, akisisitiza kuwa kigezo kikubwa ni mtoto kutoka katika mazingira magumu.

Sauti ya 2: Dorcas Jackson, Meneja wa Kituo

Akizungumzia umuhimu wa kufadhili watoto wenye uhitaji, Mchungaji Enoshi Aloyce wa FPCT Mtwara ameitaka jamii kuwa na amani na furaha kwa kushika mkono wa mtoto mwenye uhitaji ili aweze kupata elimu na kujikwamua katika umasikini.

Sauti: Mchungaji Enoshi Aloyce, FPCT Mtwara

Nao baadhi ya wazazi pamoja na watoto wanufaika wa kituo hicho wamekishukuru uongozi wa kituo kwa kuendelea kuwapatia msaada na zawadi mbalimbali. Wametoa wito kwa wazazi na walezi wanaoishi katika mazingira magumu kuwapeleka watoto wao katika kituo hicho ili waweze kunufaika na huduma na misaada inayotolewa.

Sauti za baadhi ya wazazi na watoto wanufaika wa kituo hicho
Mmoja ya miongoni mwa wazazi waliojitokeza wakati wa upokeaji wa zawadi za watoto katika kituo cha maendeleo ya mtoto na vijani FPCT Mtwara(picha na Musa Mtepa)
Share:

Sikiliza jamii FM Radio

🎧 Jamii FM Live

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

Blog Archive

WAENDESHA WEBSITE

Contact Form



1 ] )[0]; $title = $recent_post['post_title']; $excerpt = wp_trim_words( $recent_post['post_content'], 20 ); $image = get_the_post_thumbnail_url( $recent_post['ID'], 'full' ); ?>