
Mh. Shamsia Mtamba ashinda kura za maoni CUF Mtwara Vijijini kwa kura 334 kati ya 374, akimuacha Abdull Mahupa nyuma kwa kura 39
Na Musa Mtepa
Aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Mtwara Vijijini, Mh. Shamsia Azizi Mtamba, ameibuka mshindi katika uchaguzi wa kura za maoni wa Chama Cha Wananchi (CUF), uliofanyika leo kwenye ukumbi wa mikutano wa Paris, mjini Mtwara.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, Msimamizi wa uchaguzi Bw. Masudi Muhina amesema jumla ya kura 374 zilipigwa ambapo Mh. Shamsia Mtamba alipata kura 334, huku mpinzani wake Abdull Bakari Mahupa akijizolea kura 39. Kura moja iliharibika.
Akizungumza baada ya kutangazwa kwa matokeo, Abdull Mahupa alikubali kushindwa na kumpongeza Mh. Shamsia kwa ushindi huo. Aidha, aliwaomba wanachama wa CUF kuvunja makundi na kuungana kwa pamoja kumpa ushirikiano Shamsia katika harakati za kulirudisha jimbo hilo mikononi mwa chama katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29, 2025.

Kwa upande wake, Mh. Shamsia Mtamba amewashukuru wajumbe wa mkutano kwa kuendelea kumuamini na kumchagua tena kuwa mgombea wa jimbo hilo, huku akiwaomba kuendelea kushirikiana naye katika kampeni zijazo.
Kabla ya uchaguzi, wagombea walipata fursa ya kunadi sera zao mbele ya wajumbe wa mkutano huo, sambamba na kujibu maswali mbalimbali kutoka kwa wanachama – hatua iliyowapa nafasi ya kueleza kwa kina mikakati yao ya kuimarisha maendeleo ya jimbo la Mtwara Vijijini.






No comments:
Post a Comment