Wafanyakazi wa taasisi za redio wamekumbushwa wajibu wao kama ilivyo chombo chochote cha habari kuwa matarishi wa amani, upendo, mshikamano na kuhuisha maendeleo.
Aidha wameambiwa kwamba kwa kuwa Redio ina nguvu kuliko chombo chochote kingine duniani kwa kuwafikia watu wengi zaidi hivyo basi wanatakiwa kuwa makini wanapowafikishia wananchi taarifa.
Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe katika hotuba yake iliyosomwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Juliana Shonza katika maadhimisho ya Siku ya Redio Duniani yaliyofanyika Dodoma ambaye alitaka taarifa kwa wananchi kufikishwa bila ushabiki, chuki au kupiga chuku (kuongeza chumvi).
Alisema tasnia ya uandishi wa Habari ni tasinia adhimu sana, hivyo Waandishi wote wa Habari wanalo jukumu kubwa la kuzingatia misingi ya uandishi ambayo ni mizania (balancing), kutofungamana na upande wowote (impartiality), kutenda haki (fairness), Utu (humanity), na mwisho kabisa kuzingatia ukweli (truthness).
Siku ya Redio Duniani huadhimishwa kila mwaka duniani kote Tarehe 13 mwezi Februari ili kutambua mchango mkubwa unaotolewa na Redio mahali pote duniani.
Aliwakumbusha waandishi na wageni historia ngumu na mbaya ya namna redio zilivyotumika vibaya katika baadhi ya nchi duniani na kuleta machafuko hadi umwagaji damu.
“Hivyo niwaase tena kutumia redio hizo na vipaza sauti kwa ajili ya kutoa taarifa muhimu juu ya masuala ya kilimo na ufugaji, majanga mbalimbali, elimu juu ya sera na sheria mbalimbali za nchi, masuala ya afya kwa jamii na elimu. Na kwa kufanya hivyo tu, ndipo tutakuwa tumeitendea haki tasnia hii.” alisema Dk. Shonza.
Aidha alipongeza kauli mbiu ya mwaka huu Redio na Michezo na kutoa rai kwa waandishi wote wa habari kudumisha mila na desturi za Kitanzania na kuongea Kiswahili fasaha bila kuchanganya na lugha zingine kama Kiingereza maarufu kama Kiswanglish.
Aidha Waziri Mwakyembe alishukuru Shirika la UNESCO na Mtandao wa Redio Jamii Tanzania (TADIO) kwa kuwezesha siku ya redio na kusema atatafakari hoja zote zilizowasilsihwa kwake.
Naye Katibu wa Mtadao wa Radio Jamii (TADIO), Marco Mipawa akisoma hotuba kwa niaba ya Mwenyekiti wa mtandao huo, Prosper Kwigize alitaka serikali kuhakikisha kwamba urasimu unaondolewa kwenye utoaji wa taarifa kwa umma ili kuwezesha kufanyika kwa vipindi mbalimbali vya habari.
Alitaka Tamisemi kuweka utaratibu wa utoaji habari katika mfumo rahisi ili wananchi wafahamu kinachotekelezwa na serikali yao. Aidha maafisa habari walioajiriwa wapewe mamlaka na wawezeshwe kufahamu kinachofanywa na serikali na wawe na ruhusa ya kutoa taarifa kwa vyombo vya habari katika maeneo yao.
Aidha alisema kutokana kutokuwa na vyanzo vya mapato ya uhakika serikali ingeangalia suala la kodi na ushuru mbalimbali ili kusaidia Redio za Jamii kutolipia huduma za Radio.
Pia amesema sheria zilizopo ukilinganisha na mazingira halisi ya kazi ya mwanahabari, mfano sheria ya Takwimu, sheria ya huduma za habari, sheria ya makosa ya mtandao kumeshabibisha tasnia ya habari na utangazaji kuwa katika mashaka zaidi kuliko kipindi kilichopita.
Pia ameitaka Serikali kutoa Ruzuku ya elimu au mafunzo ya kitaaluma kwa wanahabari ili kuwawezesha kukidhi vigezo vya kisheria ifikapo 2021
Kaimu Mkuu wa Ofisi za Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) nchini, Faith Shayo amewataka waandishi na watangazaji kutumia redio kwa manufaa ya taifa kuleta mshikamano na pia kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.
Aidha alikumbusha historia ya redio na kazi iliyofanya duniani na kusema kwamba umuhimu wa radio upo wazi na kutaka wahusika kuzitumia kwa manufaa ya umma unaowazunguka.
Naye Mkuu wa Mawasiliano na Habari wa Tume ya Taifa ya Unesco (NATCOM), Christina Musaroche akitoa neno la shukrani kwa niaba ya Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume hiyo Dk Moshi Kimizi, alitaka serikali na vyombo vya habari kushirikiana katika kuhimiza michezo kwa kuwa ndicho kinachowaleta wananchi pamoja.
Alisema anadhani redio na serikali vitaona njia bora ya kutangaza michezo kwa manufaa ya taifa.
Awali akimkaribisha Mgeni rasmi Naibu Waziri wa Habari Mh. Shonza, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Binilith Mahenge amesema Unesco inafanya kazi nzuri sana kwa kuwekeza kwenye vyombo vya Habari na kuvitaka vyombo hivyo kuitangaza Dodoma na fursa zake kwa sababu ndio makao makuu ya nchi.
Aidha aliitaka Redio kutangaza fursa zote ambazo zipo Dodoma ili wafanyakazi na wafanyabiashara wanaohamia Dodoma kujua wanapata wapi mahitaji yao yakiwemo Makazi, Maji, Chakula, Elimu na kadhalika.
Alitaka vyombo hivyo kuvutia wawekezaji ili mji huo uwe kweli katika karne ya 21 na makao makuu ya nchi.
Mtangazaji Mkongwe wa Habari za Michezo nchini, Abdallah Majura amesema pamoja na kwamba waandishi wanatangaza vipindi vya michezo lakini maudhui hayakidhi na kuvutia vile inavyostahili akitoa mfano hai wakati akichangia kwa nini waandishi wengi hawaandiki habari za michezo. Majura amesema yeye mwenyewe amewahi kupata #tuzo mbili kwa ajili ya vipindi vya michezo.






No comments:
Post a Comment