• VIPINDI VYA ELIMU HASA KILIMO

    Tuna vipindi mbalimbali vinavyohamasisha jamii katika kilimo cha Korosho, ufuta na Mhogo. tunaendelea na jamii inafurahia uwepo wa vipindi kwa sababu wanakutana na wataalamu moja kwa moja

  • SAUTI ZA WANAJAMII HUSIKIKA

    Sauti ni muhimu hasa unapohudumia jamii ya vijijini, wasikilizaji hupenda kusikia sauti zao kwakua watu wao wanawafahamu, hivyo huwa kivutio kwako na ni rahisi jamii kuamini kuwa mpo pamoja nao

  • MICHEZO MBALIMBALI

    Afya ni sehemu ya vipindi vyetu kwenye radio, hii husaidia kuwapa fursa watu wanaopenda michezo kuwa pamoja na kubadirishana mawazo, michezo hujenga urafiki na undugu baina mwa jamii

  • WATOTO KATIKA RADIO

    Hupenda kushiriki na hujiona sehemu ya radio kwa kuwa huishi katika jamii, kipindi cha watoto kimekuwa kikifuatiliwa na watu wazima kwasababu kuu moja tu, watoto waishio vijijini huwa hawapewi kipaumbele kama tulivyofanya Jamii fm

  • SIKIKA KATIKA RADIO

    Kipengere hiki hutoa fursa kwa wanajamii wanaotuzunguka kuongea moja kwa moja na kueleza hoja zao ambazo baadae hufuatiliwa kwa undani

Waziri Nanauka azindua Jukwaa la vijana Mtwara

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Mhe. Dkt. Joel Nanauka,akiwa katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha SAUT tawi la Mtwara tayari kwa uzinduzi wa jukwaa la vijana kwa mkoa wa Mtwara(Picha na Musa Mtepa)

Waziri  Nanauka amewahimiza vijana kujiandaa kuchangamkia fursa za maendeleo wakati wa uzinduzi wa Vijana Platform Mtwara

Na Musa Mtepa

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Maendeleo ya Vijana, Mhe. Dkt. Joel Nanauka, amewataka vijana kuwa na maandalizi madhubuti ili kuchangamkia fursa zinazotolewa na wadau mbalimbali pamoja na wizara hiyo.

Ametoa kauli hiyo leo Machi 2, 2026 wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Vijana (Vijana Platform) mkoani Mtwara, uliofanyika katika viwanja vya Chuo cha Stella Maris, Mtwara.

Waziri Nanauka amesema jukwaa hilo linalenga kufungua ndoto za vijana na kuwawezesha kuchangamkia fursa za maendeleo, akisisitiza kuwa maandalizi ni msingi wa mafanikio.

Sauti ya Dkt Joel Nanauka waziri wa vijana

Akizungumzia shilingi bilioni 200 zilizotolewa na serikali kwa Wizara ya Maendeleo ya Vijana kwa ajili ya kusimamia mikopo ya vijana na wanawake, Waziri Nanauka amewataka vijana kufuatilia taarifa sahihi kupitia ngazi za kata hadi halmashauri ili kufahamu taratibu za mikopo hiyo.

Sauti ya Dkt Joel Nanauka waziri wa vijana

Aidha, Dkt. Nanauka amezielekeza halmashauri zote nchini kuhakikisha vijana wanapewa kipaumbele katika utoaji wa tenda za huduma mbalimbali za kiserikali, ikiwemo shughuli za Mwenge.

Sauti ya Dkt Joel Nanauka waziri wa vijana

Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Donald Msengi, amesema mkoa umejipanga kuhakikisha vijana wanachangamkia fursa za kiuchumi zikiwemo kilimo, uchumi wa bluu na miradi mingine ya kimkakati inayotekelezwa mkoani humo.

Sauti ya Dolnad Msengi mkuu wa mkoa wa Mtwara
Share:

Trilioni moja kukuza gesi asilia Mtwara

 

Mtambo wa uchimbaji Gesi Ardhini ukifanyakazi katika kitalu cha Mnazi Bay Msimbati ikiwa miongoni mwa visima vitatu vinavyotarajiwa kuchimba katika eneo hilo(Picha na Musa Mtepa)

Serikali yawekeza zaidi ya trilioni moja kwenye miradi ya gesi Mtwara, ikilenga kuimarisha upatikanaji wa umeme na kukuza viwanda nchini

Na Musa Mtepa

Zidi ya shilingi trilioni moja za Kitanzania zimewekezwa katika sekta ya gesi asilia kupitia miradi ya uchimbaji katika visima vya Mnazi Bay, Ntorya pamoja na mradi wa ujenzi wa bomba la gesi kutoka Ntorya hadi bomba kuu la Madimba, hatua inayolenga kuimarisha upatikanaji wa nishati nchini.

Hayo yamesemwa Februari 27, 2026 na Waziri wa Nishati,  Mhe. Deogratius Ndejembi, alipofanya ziara na kuzindua uchimbaji wa kisima kipya cha gesi asilia katika eneo la Mnazi Bay, kata ya Msimbati, wilayani na mkoani Mtwara.

Waziri Ndejembi amesema fedha hizo za Serikali, zaidi ya trilioni moja, zinalenga kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa umeme unaotokana na gesi pamoja na kukuza sekta ya viwanda na uzalishaji nchini.

Sauti ya Deogratius Ndejembi, Waziri wa Nishati

Aidha, Waziri Ndejembi amesisitiza kuongeza kasi ya uchimbaji katika maeneo mengine ili vitalu vilivyopo vianze kuzalisha badala ya kubaki kwenye hatua za maandalizi pekee.

Sauti ya Deogratius Ndejembi, Waziri wa Nishati

Akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Meneja Mradi Mhandisi Coletha Selsi amesema kitalu hicho kinatarajiwa kuongeza zaidi ya futi za ujazo milioni 55 za gesi asilia kwa siku.

Sauti ya Coletha Selsi, Mradi uchimbaji kitalu cha Mnazi Bay

Ameongeza kuwa katika kitalu hicho, Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) linamiliki asilimia 40 huku M & P ikimiliki asilimia 60. Makubaliano yao yanahusisha uchimbaji wa visima vitatu — viwili vya nyongeza na kimoja cha utafutaji katika shapu jipya la Kasa.

Sauti ya Coletha Selsi, Mradi uchimbaji kitalu cha Mnazi Bay

Ziara hiyo ya siku mbili ya Waziri Ndejembi mkoani Mtwara ilianza Februari 27 na kuhitimishwa Februari 28, 2026. Katika ziara hiyo, alizindua uchimbaji wa kitalu kipya cha Mnazi Bay, kuweka jiwe la msingi mradi wa bomba la gesi kutoka Ntorya kwenda bomba kuu la Madimba, pamoja na kutembelea mradi wa utafutaji wa vyanzo vipya vya gesi katika kijiji cha Hiari (Dangote), unaotekelezwa katika vijiji 40 vya mikoa ya Mtwara na Lindi.

Share:

Waziri Ndejembi ataka mradi wa Gesi Ntorya ukamilike kwa wakati

 

Picha na Mchoro wa mradi wa uchimbaji na ujenzi wa bomba la Gesi asilia kutoka Ntorya kuelekea Bomba kuu la Madimba (Picha na Musa Mtepa)

Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, amemtaka mkandarasi kukamilisha mradi wa bomba la gesi Ntorya–Madimba ifikapo Septemba 2026

Na Musa Mtepa

Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi, amemtaka mkandarasi anayetekeleza mradi wa uchimbaji na ujenzi wa bomba la kusafirishia gesi asilia kutoka Ntorya kwenda Madimba mkoani Mtwara kukamilisha mradi huo kwa wakati, ili kuendana na mahitaji ya Watanzania.

Rai hiyo ameitoa Februari 27, 2026, wakati wa uwekaji wa jiwe la msingi la mradi wa uchimbaji na usambazaji wa bomba la gesi asilia uliofanyika katika eneo la Ntorya, lililopo kijiji cha Namahyakati Barabarani, kata ya Nanguruwe, mkoani Mtwara.

Ndejembi amesema lengo la wizara ni kuhakikisha kuwa ifikapo Septemba 2026, visima hivyo vinaanza kuzalisha gesi na kuungwa katika bomba kuu la Madimba. Amesisitiza kuwa mkandarasi hana budi kuhakikisha mradi unatekelezwa kwa wakati na kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa.

Sauti ya Deogratius Ndejembi, Waziri wa Nishati

Aidha, Ndejembi amesema ili kufanikisha hilo kunahitajika usimamizi wa hali ya juu kutoka kwa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), kwa kuwepo eneo la mradi muda wote, ili wakati utakapofika mradi huo uweze kuanza kama ilivyopangwa.

Sauti ya 2 Deogratius Ndejembi, Waziri wa Nishati

Akizungumzia hali ya utekelezaji wa mradi huo, Mjiolojia Mwandamizi ambaye pia ni Meneja wa Mradi wa Ntorya kwa upande wa mkondo wa juu, Patrick Kabwe, amesema utekelezaji ulianza mwaka 2005 baada ya kusainiwa kwa mkataba kati ya TPDC, Ndovu Resources ya Uingereza pamoja na Wizara ya Nishati na Madini kwa wakati huo.

Amesema mwaka 2010 walichimba kisima cha Ntorya namba moja na kufanikiwa kugundua gesi ambayo sasa inatarajiwa kuchimbwa na kuungwa katika bomba kuu la Madimba.

Sauti ya Patrick Kabwe, Meneja wa Mradi wa Ntorya

Akimkaribisha Waziri wa Nishati, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Dkt. James Mataragio, amesema kitalu cha gesi cha Ntorya ni kitalu kipya kitakachoongeza upatikanaji wa gesi, huku mahitaji yake yakiendelea kuongezeka siku hadi siku kutoka kwa wananchi.

Ameongeza kuwa Wizara ya Nishati kupitia TPDC imejipanga kuhakikisha inachimba na kuzalisha gesi ya kutosha kutoka maeneo mbalimbali nchini ili kukidhi mahitaji ya viwanda na matumizi ya wananchi.

Sauti ya Dkt. James Mataragio, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati

Kukamilika kwa visima vitatu vya gesi vinavyochimbwa katika eneo la Ntorya — Ntorya namba moja, Ntorya namba mbili na Ntorya namba tatu — kunatarajiwa kuongeza uzalishaji wa gesi asilia kwa takribani futi za ujazo milioni 60 kwa siku katika uzalishaji wa gesi nchini.

Baada ya uzinduzi huo, Waziri wa Nishati alitembelea eneo la Mnazi Bay, ambapo kuna uchimbaji wa kisima kipya ambacho kikikamilika kitaongeza takribani futi za ujazo milioni 45 za gesi asilia kwa siku. Kwa sasa, uzalishaji wa gesi kutoka Mnazi Bay ni takribani futi za ujazo milioni ni 90 – 100 za gesi asilia kwa siku (Million Standard Cubic Feet per Day) MMscf/d).

Share:

Soko la Embe nje ya nchi kufikia Dola Bilioni 75

 

Mwonekano wa Embe mbichi zikiwa zimedondoshwa mtini (Picha kwa msaada wa mtandao)

Mkurugenzi wa AGCOT na wizara ya kilimo wametaka wadau kukuza zao la embe, kuongeza tija, kuuza nje, na kuwapatia wakulima zana za kisasa ili kuongeza mapato na maendeleo ya kilimo

Na Musa Mtepa

Mkurugenzi Mkuu wa AGCOT, Geoffrey Kirenga, amewahimiza wadau wa kilimo kuendeleza na kuinua zao la embe katika soko la ndani na la kimataifa ili kuongeza kipato cha wakulima na kupunguza utegemezi wa zao la korosho pekee.

Akizungumza  Februari 18, 2026, baada ya Warsha ya Wadau wa Kilimo iliyolenga kujenga uelewa wa pamoja kuhusu uendelezaji na ukuzaji wa Shoroba za Kilimo kwa mikoa ya Ruvuma, Lindi na Mtwara, iliyofanyika mjini Mtwara, Kirenga amesema kuna fursa kubwa katika uzalishaji wa embe kwa kuongeza thamani na kuuza nje ya nchi, hatua itakayoongeza mapato ya fedha za kigeni kwa wakulima na taifa kwa ujumla.

Sauti ya Geoffrey Kirenga, Mkurugenzi Mkuu wa AGCOT.

Kirenga ameeleza kuwa endapo zao la embe nchini litaendelezwa ipasavyo, soko lake Duniani linaweza kufikia zaidi ya Dola za Kimarekani bilioni 75 kwa mwaka, sawa na zaidi ya shilingi trilioni 187.5 za Tanzania, kiasi kinachokadiriwa kuwa takribani mara tatu ya mapato yanayotokana na zao la korosho.

Sauti ya Geoffrey Kirenga, Mkurugenzi Mkuu wa AGCOT.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Ofisi ya Mageuzi ya Kilimo katika Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Elizabeth Misokia, amesema shoroba za kilimo zimeanzishwa kwa lengo la kuweka mikakati madhubuti ya kukuza sekta ya kilimo kupitia ongezeko la uzalishaji, ajira na mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara na wakulima ili waweze kunufaika kibiashara.

Sauti ya Bi. Elizabeth Misokia, Mkurugenzi wa Ofisi ya Mageuzi ya Kilimo

Aidha, Misokia amesema licha ya mipango thabiti inayotekelezwa na Serikali, bado wakulima wengi wanatumia zana duni kama majembe ya mkono. Hivyo, Serikali imejipanga kuwapatia wakulima zana za kisasa zikiwemo matrekta, elimu ya kilimo bora pamoja na mbegu bora ili kuongeza tija katika uzalishaji.

Sauti ya Bi. Elizabeth Misokia, Mkurugenzi wa Ofisi ya Mageuzi ya Kilimo

Akizungumzia changamoto ya kilimo kinachotegemea mvua, Misokia amesema Serikali inapanga kuboresha na kuongeza mabwawa ya maji, kuimarisha uhifadhi wa rasilimali za maji, pamoja na kushirikiana na sekta binafsi ili kuwawezesha wakulima kuendesha kilimo cha kisasa chenye miundombinu rafiki kwa uzalishaji wa mwaka mzima.

Sauti ya Bi. Elizabeth Misokia, Mkurugenzi wa Ofisi ya Mageuzi ya Kilimo
Share:

SIDO Mtwara yawataka wajasiriamali kukuza biashara kidijitali

 

Mkuu wa wilaya ya Mtwara Abdalla Mwaipaya akizungumza wakati ya mafunzo ya uingezaji thamani uliofanyika february 24,2026 mjini Mtwara(Picha na Gregory Milanzi)

Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Abdallah Mwaipaya, amewahimiza wajasiriamali kuongeza thamani ya bidhaa na kutumia teknolojia, ikiwemo akili mnemba, kukuza biashara zao. Mafunzo hayo yaliandaliwa na SIDO kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kuwawezesha kibiashara

Na Gregory Millanzi

Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Abdallah Mwaipaya, amewataka wajasiriamali kuongeza thamani ya bidhaa zao ili kuongeza kipato, pamoja na kutumia mitandao ya kijamii kujitangaza na kuendana na kasi ya mabadiliko ya teknolojia.

Mwaipaya ameyasema hayo Februari 24, 2026, wakati akifungua semina ya utambuzi wa bidhaa, viwanda na matumizi ya akili mnemba (Artificial Intelligence), iliyofanyika katika Ukumbi wa Benjamini Mkapa, Chuo Kikuu cha MUST Mtwara (zamani Chuo cha Ualimu TTC Kawaida).

Sauti ya Abdallah Mwaipaya – Mkuu wa Wilaya ya Mtwara

Kwa upande wake, Meneja wa Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo (SIDO) Mkoa wa Mtwara, Merina Mkuchu, amesema lengo la semina hiyo ni kuwatambua wajasiriamali wa Manispaa ya Mtwara na kuwapatia elimu ya kufanya biashara kidijitali badala ya kufanya biashara kwa mazoea.

Mkuchu ameongeza kuwa kwa sasa wanaandaa kanzidata ya kuwatambua wajasiriamali hao ili kuwaunganisha na wadau mbalimbali wanaofika Mtwara kutafuta washirika wa biashara. Pia, SIDO inaandaa kongani la viwanda katika kila wilaya kwa lengo la kuwaunganisha wajasiriamali na kukuza ushirikiano miongoni mwao.

Sauti ya Merina Mkuchu – Meneja SIDO Mkoa wa Mtwara

Naye Afisa Uhusiano kwa Umma kutoka Tume ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH), Feisal Abdul, amewahimiza wajasiriamali kuchangamkia fursa zinazotolewa na Serikali kupitia Mfuko wa Uendelezaji Ubunifu (Samia Fund), unaolenga kuwajengea uwezo na kuwapatia ruzuku za kuendeleza bunifu zao.

Sauti ya Feisal Abdul – Afisa Uhusiano COSTECH

Aidha, kampuni ya Scan Code imetoa mafunzo kwa wajasiriamali wa Mtwara kuhusu matumizi ya Scan Code na akili mnemba katika kujitangaza na kupanua masoko ya biashara zao.

Abdulwahid Khamis, mkufunzi kutoka Scan Code, ameeleza faida za teknolojia hiyo na namna inavyoweza kuwasaidia wajasiriamali kuongeza wigo wa soko na mapato.

Sauti ya Abdulwahid Khamis – Mtaalamu wa Mafunzo kutoka Scan Code
Share:

Vijana Mtwara wahimizwa maadili kulinda amani nchini

 

Vijana wa Skauti wakiwa katika maandamano ya kuadhimisha siku ya Skauti Duniani ambayo kitaifa yamefanyika katika viwanja vya Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara (Picha na Musa Mtepa)

Vijana wamehimizwa kutumia mitandao kwa maadili na kulinda amani wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Skauti Duniani yaliyofanyika Mtwara , yakikumbuka miaka 160 ya Robert Stephenson Baden-Powell

Na Musa Mtepa

Vijana wametakiwa kutumia mitandao ya kijamii kwa kuzingatia maadili, tamaduni na mila za Kitanzania, na kuitumia kwa manufaa yao binafsi pamoja na taifa kwa ujumla. Pia wametakiwa kuachana na maudhui yanayoharibu maadili, utu, tunu za taifa, pamoja na yale yanayochochea uvunjifu wa amani.

Nasaha hizo zimetolewa leo Februari 22, 2026 na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mtwara , ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Bi. Zainab Telack, wakati wa maadhimisho ya Siku ya Skauti Duniani yaliyofanyika kitaifa katika viwanja vya Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara.

Bi. Telack amewataka vijana kutumia teknolojia kwa hekima na busara, pamoja na kupambanua maudhui yanayopatikana kwenye mitandao ya kijamii, na kuachana na yale yote yanayoharibu imani za dini, maadili na tamaduni za Kitanzania.

Sauti ya Bi. Zainab Telack, Mkuu wa Mkoa wa Lindi

Aidha, Bi. Telack ameendelea kusisitiza umuhimu wa vijana kuipenda na kuilinda amani iliyopo nchini kwa kuwa na uzalendo wa kweli kwa Tanzania. Alisema hakuna nchi nyingine kwao zaidi ya Tanzania, hivyo ni wajibu wa kila kijana kuhakikisha anailinda na kuipambania nchi yake.

Sauti ya Bi. Zainab Telack, Mkuu wa Mkoa wa Lindi

Akisoma risala mbele ya mgeni rasmi, Sarah Vanessa, mwakilishi wa Skauti Mkoa wa Mtwara, amesema pamoja na mafanikio makubwa yaliyopatikana kupitia Skauti bado kuna changamoto mbalimbali zinazowakabili zikiwemo ufinyu wa bajeti ya kusaidia vijana wa skauti kutekeleza miradi ya uzalishaji mali, pamoja na ukosefu wa vifaa vya uokoaji kwa timu za maafa katika wilaya na mikoa.

Sauti ya Sarah Vanessa, Mwakilishi wa Skauti Mkoa wa Mtwara

Akitoa salamu kwa niaba ya Bodi ya Skauti Tanzania, mwakilishi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Ndugu Lazaro Mkeni, amesema wizara itaendelea kusimama pamoja na Chama cha Skauti Tanzania kuhakikisha misingi ya kuanzishwa kwa chama hicho inalindwa na kuimarishwa. Ameongeza kuwa wizara ipo tayari kutoa msaada pale inapobidi ili kuhakikisha misingi hiyo inasimamiwa ipasavyo.

Sauti ya Lazaro Mkeni, Mwakilishi kutoka Wizara ya Elimu

Kwa upande wake, Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mtwara, Komredi Ibrahim Mjanaheri Ibrahim, amewapongeza waandaaji wa maadhimisho hayo,huku akitoa rai kwa vijana kuendelea kudumisha amani na kuachana na mtu yeyote anayetaka kuivuruga amani ya nchi.

Sauti ya Ibrahim Mjanaheri Ibrahim, Katibu wa CCM Mkoa wa Mtwara

Maadhimisho ya Siku ya Skauti Duniani Kitaifa kwa mwaka 2026 yamefanyika katika viwanja vya Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara, yakiwa na kaulimbiu isemayo: “Elimu Bunifu na Stadi za Kidijitali kwa Maendeleo Endelevu ya Vijana.”

Maadhimisho hayo ni kumbukizi ya miaka 160 tangu kuzaliwa kwa mwanzilishi wa Skauti Duniani, Robert Stephenson Baden-Powell, mzaliwa wa Uingereza, aliyezaliwa Februari 22, 1857. Alianzisha Skauti mwaka 1907 na baadaye mwaka 1908 akaandika kitabu maarufu kiitwacho Scouting for Boys.

Baden-Powell alianza kwa kufanya kambi ya majaribio mwaka 1907 katika Kisiwa cha Brownsea, Uingereza, ambapo alitoa mafunzo kwa vijana yenye lengo la kuwafundisha uongozi, kujitegemea, uzalendo na huduma kwa jamii. Harakati hizo zilisambaa duniani kote, kama ambavyo leo zimeadhimishwa mkoani Mtwara na Tanzania kwa ujumla.

Share:

Sikiliza jamii FM Radio

🎧 Jamii FM Live

IDADI YA WASOMAJI

HABARI ZA HIVI PUNDE

Blog Archive

WAENDESHA WEBSITE

Contact Form



1 ] )[0]; $title = $recent_post['post_title']; $excerpt = wp_trim_words( $recent_post['post_content'], 20 ); $image = get_the_post_thumbnail_url( $recent_post['ID'], 'full' ); ?>